Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Jamii na Makundi Maalum, Dk Dorothy Gwajima ameagiza utekelezaji wa mradi wa Kizazi Hodari unaowalenga
kuimarisha afya, ustawi na ulinzi kwa Watoto na vijana balehe wanaoishi katika mazingira hatarishi yenye Kasi kubwa ya maambukizi ya VVU.
Mradi wa Kizazi Hodari utatekelezwa kwa miaka mitano chini ya ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Watu wa Marekani (USAID) na unawalenga watoto balehe wenye umri wa kuanzia miaka 0 hadi 17.
Watekelezaji wa mradi huo ni Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Shirika la Deloitte na Shirika la kidini la ELCT.
Akizungumza jana katika uzinduzi wa mradi huo, Dk Gwajima alisema mbali na mambo yaliyoainishwa katika mradi huo utakaotekelezwa kwenye mikoa 12 nchini, ni muhimu mradi huo ukajihusisha na utoaji wa elimu sahihi ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto.
“Ni vema afua zifuatazo zikawekwa katika mpango kazi wa utekelezaji wa mradi wa Kizazi Hodari ni kutoa elimu sahihi ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto na kuendeleza programu za kuwaandaa wavulana kuwa wanaume bora wajao,”alisema.
Akielezea kuhusu mradi huo, Dk Gwajima alisema jumla ya watoto yatima na kaya 138,944 zitafikiwa na mradi huo ambao unalenga katika kuimarisha afya, ustawi na ulinzi kwa watoto na vijana balehe wanaoishi katika mazingira hatarishi.
Awali Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Deloitte, Zahra Nensi alisema mradi huo unalenga katika kuongeza wigo wa
kuwatambua watoto wenye maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) na kuwaunganisha karika huduma za afya ili kufubaza VVU.
“Kuongeza upatikanaji wa huduma za kuzuia maambukizi, kuzuia ukatili na huduma za mwitikio kwa watoto yatima na vijana,”alisema.
Pia alisema lengo jingine ni kukuza uchumi kwa ajili ya mabinti balehe na walezi wa watoto yatima na waishio mazingira hatarishi.
Mkurugenzi Mkazi wa USAID, Kate Msomvongsiri amesema hadi mwisho wa mradi huo inategemewa utakuwa umeajiri na kuwapatia huduma mbalimbali walau kwa asilimia 90 ya watoto na vijana hao.
Alisema vijana hao ni hasa kutoka kwenye vituo vya afya vinavyohudumiwa na Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kukabiliana na Ukimwi (PEPFAR).