The House of Favourite Newspapers

Usajili wa Yondani, Waipa Jeuri Polisi Tanzania

0

MARA baada ya kufanikiwa kuzinasa saini za wachezaji wa zamani wa Yanga, beki wa kati Kelvin Yondani na kiungo mkabaji Abdulaziz Makame, uongozi wa Klabu ya Polisi Tanzania umesema kutua kwa nyota hao kutaifanya timu hiyo kuwa moto msimu huu.

 

Hayo yalisemwa na Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Polisi Tanzania, Frank Lukwaro, ambaye alifunguka kuwa kabla ya wachezaji hao hawajatua klabuni hapo timu yao ilikuwa tishio kwa timu nyingi, hivyo ongezeko lao limekuja kuongeza balaa na sasa wapinzani wao wajipange kweli kwa sababu timu yao sasa imetimia kila idara.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Lukwaro alisema: “Naomba kutumia Gazeti la Championi kuwatumia salamu wapinzani wetu waliopo ligi kuu kuwa wajiandae, kwa sababu kwa sasa tunaye Yondani, yupo Makame na vijana wengine.“

 

Kwa sababu kabla hata kina Yondani hawajatua tulikuwa hatushikiki, sasa wao wametua kikosini unafikiri kutakuwa na nini tena.

 

Wajipange tu kwani hatuna mzaha tena msimu huu.”

 

Yondani amejiunga na Polisi Tanzania kwa mkataba wa mwaka mmoja akiwa mchezaji huru baada ya kuachana na Yanga mwisho wa msimu uliopita, huku Makame akijiunga na timu hiyo kwa mkopo akitokea Yanga utakaomalizika mwishoni mwa msimu huu.

Issa Liponda,Dar es Salaam

Leave A Reply