The House of Favourite Newspapers

Usihuzunike Kwa Kuachwa, Utampata Akupendae

couples

MARA nyingi baadhi ya wapenzi wanaoachwa na wenza wao wamejikuta wakigeuka kuwa watu wa huzuni katika sehemu kubwa ya maisha yao baada ya kuachwa.

Huzuni hiyo husababisha wengine kupunguza ufanisi wao wa kazi, wakati mwingine humfanya mtu kuwa dhaifu katika maamuzi na fikra zake, huku wengine wakijiona kana kwamba hawana thamani kabisa katika huu ulimwengu.

Inafikia wakati, wengine huchukia watu wa jinsia ile iliyowatenda, wanaume huwachukia sana wanawake, huku wanawake huwachukia wanaume na kuwasemea maneno mabaya, kwasababu tu ya msongo wa mawazo baada ya kuachwa na mwenza aliyempenda.

Kwa sababu ya maumivu ya kuachwa wanayoyapata, maumivu makali kuliko mtu aliyepigwa risasi au aliyejeruhiwa na kitu chenye ncha kali, hujikuta wakitamani kuishi bila kuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi kwa muda, kwa kuamini hata atakayempa nafasi kwa mara nyingine naye atamtenda kama alivyotendwa mwanzo.

Kwa wakati huo, aliyetendwa huamini hivyo na hata akishauriwa na watu wake wa karibu, kwamba mwenza aliyekuwa naye hakupangiwa na Mwenyezi Mungu huwa vigumu kuamini. Huna sababu ya kukata tamaa na kuhuzunika, jipe moyo, amini kuachwa kwako ni sehemu ya maisha ambayo ulipaswa upitie ili ujifunze maumivu hayo.

Ninachoweza kusema na kuaminini kwamba kama ipo ipo tu, msemo huu una maana ila haiwezi kuwepo kama hutafuti kile unachotaka kuwa nacho. Kama Mungu amepanga wewe kuishi au kuolewa na huyo mtu basi ndivyo itakavyokuwa hata kama ni baada ya miaka 20 ijayo, cha kufanya mwambie Mungu hivi; “kama umepanga niolewe au nimuoe mtu huyo na iwe hivyo, kama hujapanga pia nashukuru.’’

Mtu mmoja aliwahi kunisimulia namna alivyoanza uhusiano na binti mmoja wakiwa na umri mdogo, walipendana sana hadi kufikia kuwekeana ahadi ya kuoana kama wafanyavyo wengine.

Muda ulisonga wakiwa wapenzi, katikati ikatokea wakakorofishana na kuachana kabisa, kila mtu akashika hamsini zake, msichana akawa kama kaolewa na mtu mwingine. Siku moja mwenza wake wa zamani alipita jirani na anapoishi msichana yule na kumkuta akifua, alichomwambia ni kuwa ipo siku utakuwa wangu wa maisha.

Siku zikasonga wakiwa mbalimbali, ikaja kutokea siku moja wakakutana na kuanzisha uhusiano mpya kwa mara nyingine tena. Lakini safari hii uhusiano wao ulikuwa wa nguvu na upendo mwingi, kila mtu akiwa na hamu ya kukutana na mwenziye kwa mara nyingine.

Ndugu, jamaa na marafiki zao waliokuwa wakifahamu walivyoanza kuwa na uhusiano na kufarakana kwao, walishangazwa jinsi walivyoweza kurudiana na kupendana kwa dhati.Watu hawa hatimaye walifanikiwa kufunga ndoa na mpaka sasa wana watoto wawili na maisha yanaendelea kwa upendo na furaha tele.

Ninaachoweza kukushauri haijalishi changamoto na misukosuko unayokutana nayo katika uhusiano wako, kama mtu uliyenaye ndiyo chaguo lako kutoka kwa Mungu, ipo siku atarejea kundini hata kama atarukaruka vipi.

Maisha ya mwanadamu ni kama kitabu kilichoandikwa tayari, kinachofanyika kwa wanadamu ni kuperuzi kurasa ili kukamilisha kile kilichoandikwa.

Leo naomba nikomee hapa, tukutane tena siku nyingine kwa Makala haya ya mahusiano kwa ajili ya kuelimishana juu ya maisha ya kila siku.

Na Gabriel Ng’osha

Kwa maoni, tembelea ukurasa wetu wa Mimi na Uhusiano kwenye Mtandao wa Kijamii wa Facebook, Insta:mimi_na_uhusiano au jiunge na Group letu la M&U WhatsApp kwa namba 0657486475.

halotel-strip-1

Comments are closed.