The House of Favourite Newspapers

UTAJIRI WA KIFO! MAMA YAMKUTA MAZITO KWA SANGOMA!

KUTAFUTA utajiri kwa njia za mkato hapa duniani kumewaponza wengi! Mama ambaye ni mfanyabiashara, Tabu Mwelege, mkazi wa Kijiji cha Kijiweni wilayani Sengerema jijini Mwanza, yamemkuta mazito akiwa kwa mganga wa kienyeji almaarufu sangoma, Risasi Jumamosi lina kisa na mkasa.

 

Tukio hilo lilijiri maeneo hayo Februari 25, mwaka huu ambapo Tabu alijikuta akiwa na majeraha kwenye sehemu mbalimbali za mwili wake na kuwa katika hali mbaya baada ya kuunguzwa kwa maji ya moto alipokwenda kwa sangoma huyo ili kukuza biashara yake na kupata mali.

 

TABU ASIMULIA MKASA

Akilisimulia Risasi Jumamosi mkasa huo akiwa katika Hospitali ya Bugando jijini hapa huku akiwa na majeraha hayo, Tabu alieleza:“Nilikuwa nafanya biashara zangu ndogondogo pale Sengerema. “Nilifanya biashara kwa muda mrefu sana bila mafanikio.

 

Siku moja nilikwenda kwa mganga wa kienyeji aliyekuja pale kijijini ili nipate dawa za kukuza biashara zangu.“Kweli nilipofika kwa huyo mganga kulekule Sengerema,nilimweleza shida zangu.“Yule mganga aliniambia kama tatizo langu ni hilo nisiwe na shida kabisa na niondoe shaka kwani nilikuwa nimefika na kila kitu kitakuwa sawa.

 

“Nakumbuka pale kwa mganga siku ile kulikuwa na watu wengine ambao walikuwa wakihudumiwa. Ilinibidi nisubiri hadi zamu yangu ilipofi ka huku nikiwa na matumaini makubwa ya kufanikisha lengo langu la kukuza biashara zangu na kupata utajiri. “Yule mganga alikuwa mgeni pale kijijini kwetu.

 

Aliniambia ananitengenezea dawa nzuri itakayonisaidia kwenye kazi zangu. “Nakumbuka aliweka mawematatu kwenye maji na kuyachemsha yale maji hadi yakachemka kabisa kama mtu anayetaka kupika ugali.“Hapo yule mganga aliniambia nilale chali ambapo aliniwekea jiwe la kwanza kifuani. “Baada ya kuniwekea lile jiwe la moto sana, aliniwekea yale mawe aliyokuwa akichemshia maji.

 

“Aliendelea hivyo hadi mawe yote matatu yakaisha.Wakati huo nilikuwa naumia sana, lakini nilikuwa navumilia. “Baada ya lile jiwe la tatu,ndipo nikaanza kusikia maumivu makali mno ambayo sijawahi kuyapata. Wakati huo nilikuwa nimefunikwa shuka ili ule mvuke usitoke nje.

 

Hapo ndipo nikajikuta nimeungua mikono, kifuani, shingoni na mdomoni, nikapewa huduma ya kwanza ikiwemo kukimbizwa hospitalini kule Sengerema kabla ya kuhamishiwa hapa, lakini namshukuru Mungu naendelea vizuri na matibabu hapa Bugando,” alisimulia Tabu akiugulia maumivu makali hivyo kushindwa kuendelea na mahojiano na Gazeti la Risasi Jumamosi.

 

MWANAYE NAYE

Baada ya mama mtu kuishia hapo, mwanaye Tatu Kakulu aliendelea kusimulia kuwa, baada ya kupata taarifa ya mama yao kuunguzwa na mganga huyo walikwenda kumchukua kasha kumuwahisha hospitalini. Alisema baada ya kuhamishiwa Hospitali ya Bugando, mama yake anaendelea kupatiwa matibabu na hali yake inaendelea vizuri.

 

SANGOMA ATIMKA,ASAKWA

Alipoulizwa kilichompata mganga huyo baada ya kutekeleza uhalifu huo, Tatu alisema kuwa,sangoma huyo alitimkia kusikojulikana kwani alikuwa mgeni kijijini hapo na alifi ka pale kwa ajili ya kutoa huduma ya uganga tu. Alisema kuwa, tukio hilo walikwenda kuliripoti kwenye Kituo cha Polisi cha Katunguru wilayani Sengerema ambapoanasakwa na polisi.

 

KAMANDA MSANGI

Risasi Jumamosi lilimtafuta Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, ACP Ahmed Msangi ili kuthibitisha tukiohilo lakini jitihada ziligonga mwamba baada ya simu yake kuita bila kupokelewa

STORI: IDD MUMBA, MWANZA

VIDEO: MSIKIE MAGUFULI AKIFUNGUKA

Comments are closed.