The House of Favourite Newspapers

Utatakaje upendwe wakati mwenyewe hujipendi?

0

blackcouple-bedsmileUhali gani msomaji wangu wa kona hii nzuri? Ni matumaini yangu kwamba u mzima wa afya njema. Nakuka-ribisha kwa moyo mku-njufu kwenye busati letu, mahali tunapo-juzana na kuelimisha mambo mbalimbali yahusuyo uhusiano wa kimapenzi.

Kwa muda mrefu sasa nimekuwa nikipokea malalamiko ya mara kwa mara kutoka kwa watu waliopo kwenye uhusiano, wakiwalalamikia wenzi wao kwamba hawawaoneshi mapenzi ya dhati, wanawaumiza mara kwa mara na kuwatesa kimapenzi.

Si ajabu hata wewe msomaji wangu, kwa namna moja au nyingine umewahi kuhisi kwamba mwenzi wako hakupendi, anakutumia na ipo siku atakukimbia na kwenda kwa mwingine.

Kutokana na wingi wa malalamiko hayo, kutoka pande zote, wanawake na wanaume, waliopo kwenye ndoa au waliopo kwenye uhusiano wa kimapenzi, nimeamua niilete mada hii mezani ili kwa pamoja tujadiliane.

Upo msemo maarufu kwamba kumpenda mtu kwa dhati, hakutokei tu kama bahati mbaya! Kupenda ni uamuzi kutoka ndani ya moyo wako, ambao pengine unaufikia mwenyewe ukiwa unajua au ukiwa hujui.

Maana yangu ni kwamba, haiwezi kutokea ukaanza tu kumpenda mtu bila kuwa na sababu ambazo zimekuvutia kwake. Wapo wanaovutiwa na sifa za nje, wapo wanaovutiwa na sifa za ndani na wapo wanaovutiwa na sifa zote. Ikumbukwe hapa sizungumzii KUTAMANI, nazungumzia KUPENDA!

Sasa kama tunakubaliana kwamba kupenda ni uamuzi wa moyo, swali ambalo kila mmoja anatakiwa kujiuliza, wakati unavutiwa kumpenda mtu fulani kwa jinsi alivyo, wewe mwenyewe unajipenda?

Unaweza kumpenda mtu kwa sababu ana tabia nzuri, mtulivu, anajiheshimu, anafikiria maisha na sifa nyingine kama hizo lakini je, umewahi kujiuliza na wewe unatakiwa kuwa na sifa gani ili yule unayempenda avutiwe na wewe na hata mkiingia kwenye uhusiano aendelee kukupenda siku zote za maisha yenu?

Jambo ambalo watu wengi hawalijui, upendo huwa unaanzia ndani yako kwanza. Haiwezekani ukampenda mwenzi wako, ukamtimizia kila anachokitaka, ukamfanyia mambo yatakayomfurahisha kama wewe mwenyewe hujipendi.

Huenda ukajiuliza kujipenda maana yake ni nini? Jibu lake ni rahisi sana. Unapompenda mtu mwingine, unakuwa unatamani sana kumfanya afurahi kwa kumfanyia mambo mazuri, kama kumnunulia zawadi nzuri, kumwambia maneno mazuri, kumpa msaada wa aina yoyote pale anapohitaji na kumfanya ajisikie kuwa na amani ndani ya moyo wake.

Sasa kabla ya kuanza kumfanyia mwingine mambo hayo ili mapenzi yanayotoka ndani ya moyo wako yawe ya kweli ni lazima kwanza ujifanyie mambo hayo wewe mwenyewe. Anza kwa kujipenda, jifanyie mambo mazuri wewe mwenyewe, jinunulie zawadi nzuri kama nguo nzuri, manukato, simu na mahitaji mengine muhimu.

Kwa kuwa utakuwa umejua maana ya kujipenda naamini utampenda mwenzi wako pia.

Kama una maoni au ushauri, nitumie meseji (SMS tu) kwa namba za hapo juu. Itaendelea wiki ijayo.

Usikose kuhudhuria Semina ya Mimi na Uhusiano (M&U). Mada kuu itakuwa ni: KUNA MAISHA NJE YA MAUMIVU YA MAPENZI. Itafanyika Agosti, 27 mwaka huu kwenye Ukumbi wa Malaika, Kijitonyama. Kwa maelezo zaidi na kufanya booking, piga simu: 0657486745 au tembelea ukurasa wa Facebook wa Mimi na Uhusiano.

Leave A Reply