The House of Favourite Newspapers

UWOYA, MOBETO GUMZO MKUTANO WA SADC

GUMZO kubwa huko mtaani pamoja na kwenye mitandao ya kijamii ni kibarua alichoomba msanii mkubwa wa filamu Bongo, Irene Uwoya cha kupokea wageni wanaokuja nchini kuhudhuria mkutano wa wakuu wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).  Mkutano huo unatarajiwa kufanyika Agosti 18 na 19 jijini Dar, ambapo staa huyo ameona usipite hivihivi bila kutengeneza kichwa cha habari kwa kuposti ujumbe ulioibua gumzo kwenye ukurasa wake wa Instagram akimuomba Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ampe kazi ya kupokea wageni.

Uwoya aliandika: “Jamani mashabiki zangu naomba mnisaidie kumuita @baba_ keagan (Paul Makonda) hapa maana huu ugeni wa SADC ndani ya mkoa wetu sijui mheshimiwa Makonda atanipa kamati gani nimsaidie.

“Ila mimi naona itanifaa ile kamati ya kumpokea Mswati (jamani kiukweli naahidi nitaliwakilisha vyema taifa na wala sitamwangusha. Au labda mkuu anipe kupokea marais, jamani naahidi sitamwangusha maana nipo vizuri, mapema nitakuwa airport na hivi uwanja ni mpya halafu mzuri balaa, nitashindwaje!”

Mbali na ujumbe huo, kuonesha kuwa hatanii, baadaye Uwoya akaandika tena: “Tishaaa baba @baba_keagan, hivi Hamisa uko wapi lakini? Fursa hii mama… ohooo…haya nikiitwa …Hamisaaa nikiitwa usilie.”

Baada ya kumwingiza Hamisa Mobeto kwenye mchongo huo, Mobeto naye akaibuka kutoka mafichoni na kuandika: “Irene… Irene…Irene… wallah nimecheka… Nasemaje; naunga mkono hoja, nipo nyuma yako.” Kufuatia kufunguka kwa mastaa hao, gumzo kubwa likaibuka ambapo wapo walioshangazwa na staili ya kuomba kazi kwenye mitandao bila kufuata taratibu.

Mdau mmoja aliandika chini ya komenti ya Uwoya: “Unajua huyu anaomba kitu siriasi lakini kikomedi. Nawaambia angemfuata Makonda na kumuomba kibarua hicho huenda angemfikiria, si naonaga wanakuwepo warembo kupokea wageni, huenda angetumia njia sahihi yeye na mwenzake Mobeto wangepata shavu.”

Mwingine aliyejitambulisha kwa jina la Jesca Joo akaandika: “Hahaa, nicheke miye, Uwoya unamuombaje mkuu kibarua kwa staili hii? Hata kama ni mimi siwapi tu.” Mbali na hao, wapo ambao waliendeleza mjadala wakisema kuwa, kama wameamua kujilipua hivyo huenda inaweza kuwa bahati yao na Makonda au wahusika wengine wakawapa kazi.

“Ni wazo zuri ambalo kama halikuwepo unaweza kushangaa Uwoya, Mobeto na hata Wema wakaonekana kwenye mapokezi na ikawa kitu kizuri tu. Ngoja tusubiri tuone,” alisema mdau mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Swedy K. Risasi Mchanganyiko lilimpigia simu Uwoya ili kujua kama alifanikiwa kupata kibarua hicho, lakini simu yetu haikupokelewa muda wote aliopigiwa.

Baadaye paparazi wetu alifanya jitihada za kumtafuta Makonda kupitia simu yake ya mkononi kujua kama ameona ujumbe wa mastaa hao lakini naye simu yake iliita muda mrefu bila kupokelewa. Mkutano huo utafanyika Agosti 18 na 19 jijini Dar es Salam ambapo marais kutoka nchini takribani 16 wanatarajiwa kuhudhuria sambamba na maafisa wengine

Comments are closed.