The House of Favourite Newspapers

Uwoya Roho Mkononi Rwanda! Anaswa na Mabaunsa

0
Muigizaji Irene Uwoya

 

Siku chache baada ya Hamad Ndikumana ‘Katauti’ kufariki dunia, imedaiwa kuwa, usalama wa mzazi mwenziye marehemu, muigizaji Irene Uwoya ambaye jana alikwea ‘pipa’ kwenda kuhani msiba nchini Rwanda ni mdogo. Uwoya ambaye alifunga ndoa na marehemu na kuishi naye kwa miaka kadhaa kabla ya kutengana, alianza kufanya mipango ya safari Jumatano iliyopita, saa chache mara baada ya kupokea taarifa za kifo hicho kilichotokea Jumanne usiku.

 

CHANZO CHAFUNGUKA

 

Kwa mujibu wa chanzo makini kutoka Rwanda, kuna kikundi cha watu ambacho kimekuwa na hasira na mrembo huyo kwa kile wanachofikiri kuwa kifo cha Ndikumana kimetokana na ‘stress’ zilizosababishwa na mrembo huyo.
“Kwa kweli huku usalama wa Uwoya ni mdogo sana maana kama unavyojua kuna mashabiki ambao walikuwa wanamkubali Ndikumana ambaye alikuwa na mchango mkubwa sana katika soka la Rwanda,” kilidai chanzo hicho.

WANAAMINI UWOYA NDIYO KIKWAZO

 

Chanzo hicho kilizidi kumwaga data kuwa, wanachoamini Warwanda hao ni kuwa kwa kiasi kikubwa Uwoya ndiyo chanzo cha Ndiku kuwa na mawazo ya muda mrefu. “Wao wanafikiri Uwoya kasababisha sana mawazo kwa Ndikumana baada ya jitihada za makusudi za kuirudisha ndoa yao kufanyika bila mafanikio. Wanaamini Ndiku alikuwa anampenda sana Uwoya. “Wanaamini Uwoya ndiye alikuwa hataki suluhu na mumewe. Sasa hilo linawafanya mashabiki hao kutangaza hali ya hatari kwa mrembo huyo endapo tu akikanyaga ardhi ya Rwanda,” kilidai chanzo hicho.

 

UWOYA AAHIRISHA SAFARI

Awali, chanzo kilicho karibu na familia kililiambia Risasi Jumamosi kuwa, Uwoya alipanga kuondoka nchini kuelekea Rwanda Jumatano iliyopita lakini akalazimika kuahirisha safari huku vuguvugu la hofu ya kushambuliwa likitajwa. Mara baada ya kuahirisha siku hiyo, ikaelezwa kuwa huenda akasafiri kesho yake Alhamisi saa kumi lakini hata hivyo ilishindikana kwa mara nyingine.

 

AJIANDAA NA MABAUNSA

Chanzo hicho kilizidi kudai kuwa, mara baada ya kuona hivyo, Uwoya alilazimika kujiandaa na watu wake wa karibu, Kulwa Kikumba ‘Dude’, Mike Sangu na wengine ambao atawatumia kama mabaunsa wake endapo litatokea lolote pindi atakapokuwa nchini humo.

 

WENGINE WATANGULIA Ilidaiwa kuwa, jana asubuhi baadhi ya ndugu, jamaa na marafiki walitangulia kisha
mishale ya saa 10 jioni, Uwoya akiwa amevalia kininja alionekana Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere akiwa na mama yake pamoja na mtoto, Krish tayari kwa safari ya kuelekea Rwanda.

 

DUDE AFUNGUKA

 

Alipoulizwa Dude kuhusu suala la usalama na kwamba amejipangaje kwa safari hiyo, alisema kumlinda Uwoya ni muhimu lakini anaamini hakuna ubaya wowote utakaotokea maana Ndiku alikuwa ni shemeji yao hivyo wasanii watampa kampani Uwoya japo yeye kwa bahati mbaya hataweza kwenda. “Msiba wetu sote huu. Kampani kwa Uwoya ni muhimu. Ilikuwa niende lakini nimepata dharura lakini naamini hakitaharibika kitu hata kwa wasanii wenzangu watakaoambatana naye,” alisema Dude.

 

CHANZO CHA KIFO

Kwa mujibu wa taarifa za awali, Ndikumana alikuwa na tatizo la moyo ambalo ndilo
lilisababisha kifo chake mara baada ya kumaliza mazoezi ya timu yake ya Rayon Sports ambayo alikuwa akiitumikia kama kocha msaidizi.

 

TUJIKUMBUSHE

Uwoya na Ndikumana walifunga ndoa Julai 11, 2009 ambapo waliishi kwenye ndoa kwa miaka kadhaa na kufanikiwa kupata mtoto mmoja aitwaye Krish kisha baadaye wakamwagana na kila mmoja akawa anaishi kivyake. Kabla mauti hayajamkuta, Ndikumana alikaririwa akisema kuwa ameruhusu Uwoya aolewe na kwamba ameshatuma mtu nchini kwa ajili ya kushughulikia suala la kuivunja ndoa hiyo. Hivi karibuni, Uwoya alidaiwa kufunga ndoa na Dogo Janja ambapo hata hivyo, baadaye ilibainika kuwa si ndoa bali picha zilizosambaa zilikuwa ni za tamthiliya ambayo inatarajiwa kuonekana hivi karibuni.

Leave A Reply