VEE MONEY, JUX ‘LIFE STYLE’ YAO COPY & PEST YA JAY Z NA BEYONCE
MIAKA mitano iliyopita, staa wa kike wa Muziki wa Bongo Fleva, Vanessa Mdee ‘Vee Money’ pamoja na staa wa R&B, Juma Khalid ‘Jux’ hawakuwa wakijuana, kila mmoja alikuwa na maisha yake. Siku moja, Prodyuza wa Studio ya B’Hits, Pancho Latino alimuomba Vee Money kuingiza sauti kwenye wimbo wa Jux ambao alikuwa bado hajaupa jina, akamkatalia kwani hawakuwa wakijuana.
Lakini siku chache mbele, Vee Money baada ya kutembelea studio kwa lengo la kuingia nao mkataba wa kimuziki, akamuona Jux na kubadili mawazo kisha akaingiza mistari ya kurap kwenye wimbo huo uliojulikana baadaye kama Juu. 2016, katika kusherehekea siku ya kuzaliwa ya Jux, Vee Money alitumia mitandao ya kijamii kueleza kile kilichomtokea na mpenzi wake huyo kwa mara ya kwanza walipokutana kwa kuandika;
“Your boy asked me if I would spit some bars on your song. I said no. Then walked into the studio and met you and instantly had a change of heart.” Leo hii unapozungumzia ‘kapo’ ambazo pia ni wanamuziki wanaosumbua kwenye Bongo Fleva ni wazi utawataja Vee Money na Jux.
Licha ya kuwa wote wanamuziki, kapo hii imekuwa ikitembelea nyayo ‘copy & paste’ kutoka kapo ya mastaa wa muziki kutoka Marekani, Beyonce na Jay Z.
Mikito Nusunusu imekuchambulia baadhi ya Copy & Paste wanazopitia mulemule; Wamekutanishwa na muziki Vee Money alianza uhusiano wa siri na Jux mara baada ya kukutana studio, kila mmoja alikuwa akikanusha kuwa na mwenzake lakini 2014 uhusiano huo ulianza kuchomoza rasmi na mashabiki wengi wakatambua kuwa mbali na kufanya muziki pia ni wapenzi.
Kama ilivyo kwa Vee Money na Jux, Jay Z na Beyonce nao uhusiano wao ulianzia kwa siri kwenye muziki. Katika mahojiano aliyowahi kufanyiwa Jay z mwaka 2007 alisema kuwa, alikutana na Beyonce kwa mara ya kwanza miaka 10 iliyopita akiwa na miaka 18 tu. Jay Z aliliambia Jarida la Vanity Fair mara baada ya kupiga picha ya pamoja na Beyonce wakiwa na mastaa wengine kuwa, uhusiano wao wa kimapenzi ulianzia hapo.
Kama alivyofanya Jux na Vee Money kwenye biti ya pamoja lililozaa Wimbo wa Juu, Beyonce na Jay Z walifanya kolabo lao la kwanza 2002 katika Wimbo wa 03 Bonnie And Clyde ambapo mwanamama huyo alitumika kama video queen pia wakioneshana mahaba njenje.
KUMILIKI LEBO
Jux na Vee Money kila mmoja anamiliki lebo yake ambapo Jux anamiliki lebo ya mavazi ya kike na kiume iitwayo Afican Boy wakati Vee Money anamiliki lebo ya muziki iitwayo Mdee Music ikiwa na wasanii watatu, yeye mwenyewe, mdogo wake, Mimi Mars pamoja na Brian Simba.
Kuonesha kuwa ni copy na pest, Jay Z anamiliki lebo ya mavazi ya kiume na kike iitwayo Rocawear pamoja na lebo ya wasanii ya Roc Nation iliyo na mastaa kibao kama vile T.I, Fat Joe na Remy Ma. Upande wa Beyonce anamiliki lebo ya mavazi ya ‘gym’ iitwayo Ivy Park.
ZIARA YA PAMOJA
Kabla ya kuanza ziara ya pamoja wakiwa kama kapo walioiita On The Run II Tour (OTR II), wawili hao waliingia studio na kutoa albamu ya pamoja ya Everything is Love ikiwa na nyimbo tisa. Katika Ziara ya OTR II, Beyonce na Jay Z wamekuwa wakiwatumia wasanii wengi walioshirikiana nao katika albamu hiyo kama vile Quavo na Offset kutoka Kundi la Migos, Ty Dolla Sign na Pharrell Williams.
Upande wa Jux na Vee Money nao walichukua wazo na ki-copy ambapo hivi karibuni walimaliza ziara yao wakiwa kama wapenzi walioiita In Love And Money. Katika ziara yao hiyo, wawili hao waliwatumia wasanii walioshiriki nao katika albamu zao, Money Mondays (Vee Money) na The Love (Jux).
KILA MMOJA KIVYAKE
Kapo hizi zote hazijawahi kuungana kufanya muziki wa pamoja kwa muda mrefu zaidi ya kufanya ziara tu na baada ya hapo kila mmoja anaendelea kivyake.
Vee Money amekuwa akiingia studio na kutengeneza nyimbo kivyake vivyo hivyo kwa Jux. Jay Z ambaye ni rapa, naye amekuwa akifanya muziki kama ‘solo’ na Beyonce anayefanya R&B naye amekuwa akifanya muziki kivyake.
MAKALA: Andrew Carlos
Comments are closed.