VETA Sasa Kuja na Zana za Kisasa za Kufundishia, Walemavu Wazidi Kupata Fursa

Chuo cha Ufundi Stadi VETA katika kusherehekea miaka 30 ya taasisi hiyo kimeahidi kufanya mabadiliko makubwa ya chuo hicho ikiwemo kuboresha zana za kufundishia na kupanga kuanza kutumia zana za kisasa pamoja na walimu wenye uwezo wa kufundisha mafunzo yanayoendana na teknolojia ya kisasa.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa Elimu ya Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Dk. Abdallah Shabani wakati akiwasilisha hoja zake kwenye mjadala uliofanyika leo kwenye kongamano la miaka 30 ya VETA yanayofanyika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar.

Dk. Abdallah akielezea baadhi ya changamoto zinazokikumba chuo hicho ni kuendelea kutumia mifumo ya kufundishia iliyopitwa na wakati kama vile matumizi ya typewriter wakati ulimwengu tuliopo sasa kila sehemu inatumika kompyuta.

Ameendelea kusema watashirikiana serikali pamoja na wadau kuhakikisha wanapata vifaa vya kisasa na walimu wenye uwezo wa kufundisha mafunzo yenye tija kwa ulimwengu wa kisasa pamoja na kuangalia suala la wenye uhitaji maalum (walemavu).

Pamoja na hayo wanahabari wetu walishuhudia mabanda ya maonesho yanayoonesha ufundi wa vitu mbalimbali ikiwemo walemavu waliowezeshwa mafunzo mbalimbali ya kuweza kuajiliwa au kujiajili.

Miongoni mwa walemavu hao ni kijana Joseph Joachim Mtei ambaye amezaliwa bila mikono lakini baada ya kupata mafunzo ya VETA sasa hivi ni msanifu majengo anayetarajia kuhitimu mafunzo yake Desemba mwaka huu. HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS NA NEEMA ADRIAN /GPL