MOSHI: Mazishi ya Mzee Philemon Ndesamburo Kiwelu, yalifanyika jana Juni 6, 2017 nyumbani kwake, KDC Moshi mkoani Kilimanjaro na kuhudhuriwa na mamia ya watu wa kaada mbalimbali.
Ndesamburo aliyewahi kuwa Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini, Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Kilimanjaro na muasisi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo, alifariki ghafla katikati ya wiki iliyopita.
Ndesamburo aliagwa katika Uwanja wa Majengo Moshi ambapo baadaye ibada ya mazishi ilifanyika katika Kanisa la KKKT, Dayosisi ya Kaskazini na kuzikwa nyumbani kwake.
Philemoni Ndesamburo atakumbukwa na mengi hasa katika siasa za mageuzi ambapo katika uchaguzi wa mwaka 2015 akiwa ni mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Kilimanjaro alisaidia kupatikana kwa madiwani wengi katika baraza la madiwani wa manispaa ya Moshi.
Ndesamburo maarufu kama Ndesa Pesa ametumia muda wake mwingi katika siasa na biashara, amefariki dunia wakati akitaka kukabidhi mchango wake kwa meya wa jiji la ARUSHA, Kalist Lazaro kwa ajili ya familia za watoto wa shule ya msingi ya Lacky Vicent waliofariki katika ajali ya gari Wilayani Karatu mkoani Arusha.