The House of Favourite Newspapers

VIDEO: Kumekucha, MNYIKA wa CHADEMA Aanika ‘Bajeti ya Nishati’


Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ambaye ni mbunge wa Kibamba Mhe. John Mnyika, leo akiongea na wanahabari jijini Dar es Salaam amesema  “Siku hizi tumewekewa utaratibu kinyume na kanuni za Kibunge ambapo Mawaziri vivuli tumepewa muongozo wa kupeleka hotuba siku moja kabla ya kuwasilisha bungeni, sisi tunadhani ni wakati muafaka hata kwa ninyi wanahabari mkaipata hotuba hiyo.

 

“Bila kusubiri bajeti ya Nishati itakayosomwa keshokutwa bungeni tunamtaka Waziri wa Nishati na Waziri wa fedha wajitokeze hadharani wawaeleze wananchi ni kiasi gani cha fedha mkandarasi wa Stiegler’s amelipwa na nani anasema uongo.

 

“Wachambuzi wa Wizara ya Nishati na Madini wakati ule walisema mradi utakamilika baada ya miaka 12, sasa ni miujiza gani ambayo Serikali ya Rais Magufuli inataka kufanya ili mradi wa Stiegler’s ukamilike kwa miaka mitatu?.

 

“Serikali inalazimika kuwatoa kafara wananchi wake na inabidi ichukue hatua ya kupunguza kiwango cha fedha kwenye miradi mingine inayowagusa wananchi wa kawaida kama maji, afya na elimu ili fedha hizo zielekezwe kwenye mradi wa Stiegler’s.

“Jamii ya Kimataifa inaishangaa Serikali ya Tanzania kukata misitu na kuharibu urithi wa ulimwengu katika hifadhi ya Selous kwa sababu ya kutekeleza mradi wa Stiegler’s.

 

“Serikali imesema tathimini ya uharibifu wa kimazingira ilifanyika, hivyo basi tunaitaka Serikali ilete bungeni ripoti za tathimini hizo zilizofanywa na taasisi zenye kuheshimika na siyo ile ripoti ya Profesa iliyokataliwa.

“Sehemu kubwa ya Bomba la gesi lililojengwa kwa zaidi ya TZS trilioni 2 haitumiki mpaka sasa, tunaitaka Serikali ya Magufuli itueleze ni kwanini iliachana na mradi wa gesi na ikaanza kuzungumza mradi wa Stiegler’s na mikataba ya ujenzi wa bomba hilo iletwe bungeni.

“Spika Job Ndugai aliunda kamati kupitia masuala ya utekelezaji wa miradi ya gesi, tunataka tuelezwe juu ya utekelezaji wa uchunguzi ulioundwa kuhusu gesi, nasema haya masuala ya gesi kwa sababu mradi huu umewekwa pembeni.

“Mjadala wa Umeme, gesi na mafuta haupaswi kuwa wa Chadema peke yake bali ni wa watanzania wote, tuanze kudai mikataba ya gesi na mikataba ya Stiegler’s ipelekwe bungeni.

 

“Mjadala huu ukibaki kama jambo la Chadema peke yake, Serikali itaona kama sauti ya nyikani hivyo tuanze mjadala kupitia mitandao ya kijamii na kwenye vyombo vya habari,” amesema.

Comments are closed.