Video Queen Kaharibu Nishike Ya Bella
Video Queen aliyeshiriki video ya Christian Bella ‘Obama’ iitwayo Nishike. Bella akicheza naye.
Ni siku nyingine tena tunakutana katika kona yetu hii ya Movie and Video Review (Uchambuzi wa Filamu na Video za Kibongo). Baada ya wiki iliyopita kwenye konahii kuwepo kwa dairekta mwenzangu, Mahsein Awadh ama wengi wamezoea kumuita Dk. Cheni, leo nitakuwepo mwenyewe Dairekta wa Filamu Bongo, Adam Haji ‘Baba Haji.
Leo ningependa kuichambua video ya mwanamuziki wa dansi anayefahamika kama King of the Best Melodies, Christian Bella ‘Obama’ iitwayo Nishike ambayo ameifanyia nchini Afrika Kusini.
UZURI
Kwa upande wa audio, nisiwe mnafiki audio imesukwa, ni nzuri inagonga ngome za masikio vilivyo. Ni ngoma ambayo ukiisikia sehemu yoyote lazima unyanyuke na kuanza kuicheza. Kifupi ina amshaamsha f’lan hivi amaizing.
Wakiendelea kufanya yao.
KUPOOZA KWA VIDEO QUEEN
Naweza kusema nimekuwa mdau mkubwa wa kufuatilia Muziki wa Dansi na siyo kuusikia tu hata kuangalia video zake. Bella ni miongoni mwa
wasanii ninayevutiwa kuangalia na kusikiliza kazi zake. Video zake nyingi zina mauno ya hatari, kuanzia safu nzima ya waimbaji hadi madansa.
Akionyesha mambo yake.
Nimejaribu kuangalia video yake ya Nashindwa nikaona wadada wa Sauz wanavyokata nyonga, nilivyoiona na hii Nishike nikajua mauno yatakuwa ya kutosha lakini nimeambulia patupu.
Video queen aliyetumika katika video hii amechemka, kwanza si mchangamfu, ameshindwa hata kukatika japo kwa kujitingisha tu. Video kuanzia mwanzo hadi mwisho anauza sura tu akitembea hadi zile sehemu alizopaswa japo kukatika, kifupi ameharibu!
KIPANDE CHA FARASI
Bado nashindwa kuelewa hasa matumizi ya farasi anayeonekana katika video. Video inaanza Bella anatoka nje ya nyumba anakutana na video queen huyu na kuanza kumchezea. Ghafla Bella
amebadilisha nguo nyuma yupo mzee na farasi, hapo tena tunachanganywa tena mara mbele anaonekana akiwa na yule video queen akiwa anaelekea eneo la farasi, wanapanda lakini hatuoneshwi kama wamefika walipokuwa wakienda na matokeo yake tunaoneshwa kipande kingine wakiingia klabu tena wakiwa katika mavazi tofauti kabisa.
UMALIZIAJI
Hapa kwa mtazamo wangu, umaliziaji haukuwa mzuri sana. Asilimia kubwa ya video yake ya Nashindwa alifanya akiwa juu kabisa ya ghorofa akikatika na ndicho kilichotokea na kwenye video hii ya Nishike.
USHAURI
Video hii ilistahili kabisa kuwepo angalau madansa kama siyo wake basi hata wa huko Sauz hata mmoja ama wawili ili kunogesha maana asilimia kubwa ya wimbo huu umekaa kuchezeka.
Comments are closed.