Vingine mnashea, kwa nini simu iwe tatizo!-2
Napenda kumshukuru Mola kwa pumzi aliyonipa nikaweza kuandika makala haya na wewe msomaji ukapata kile unachokipenda.
Wiki iliyopita nilianza kuzungumzia suala la wapenzi kushea mambo mengine ila linapokuja suala la simu inakuwa ngumu kushea, jambo linalonipa wasiwasi kwa wapenzi kwa maana ya kwamba inaonesha kabisa wapenzi wengi wamechukulia mwanya huo kufanya usaliti dhidi ya wenzi wao.
Kwa wazinzi ni kama kinga kwao kwa kufichia mambo yao, hawako tayari kushika simu za wapenzi wao ili na wenzao wasipate nafasi ya kuangalia simu zao, jambo linalowafanya kuendelea kuwa huru na kusaliti.
Nimejaribu kupata baadhi ya maoni kutoka kwa wasomaji ambapo wapo waliounga mkono mada na kusema ni kweli kuna tatizo kubwa sana la kutokuwa waaminifu miongoni mwa wapenzi.
Kama mmependana na kufika hatua ya kuoana ni dhahiri kuwa mwanamke yakupasa kuachana na mambo ya ukicheche na kujenga familia iliyo bora.
Vivyo hivyo kwa mwanaume, ukiamua kupenda basi penda mmoja na mpe thamani yake kama mkeo na muweke wazi kwa kila jambo ili awe msaada mkubwa kwako kwani unapomzuia kuangalia simu yako unadhihirisha kuwa mkeo hayuko peke yake. Na hapo ndipo unapoanza kuzalisha maswali na migogoro isiyokuwa na maana katika familia yako.
Wengine wanasema kuwa mwanamke hapaswi kuangalia au kuzoea simu ya mumewe kwa sababu kuna dili nyingine za hela hapaswi kuzifahamu kwani anaweza kuona mchongo wa pesa na kuanza kupanga bajeti halafu mchongo huo ukigoma basi mwanamke anaanza migogoro.
Hivyo mwanamke ataendelea kufichwa jambo ambalo naliona ni kama hatari kwani kuna baadhi ya watu wamefariki dunia wakiwa na pesa za kutosha kwenye simu zao, wengine wemefariki wakiwa na nyaraka mbalimbali kwenye simu zao lakini kwa sababu ya usiri na usaliti wao familia yake inataabika na maisha wakati yeye amekufa simu ikiwa na pesa ya kutosha.
Anza kubadilika kama mwanamke au mwanaume unampenda mpenzi, mchumba au mkeo au mumeo basi thubutu kumfanya awe na furaha, ajue kabisa unampenda na unamwamini na yeye anakuamini na ndiyo maana huoni hatari kumuachia simu yako.
Jifunze kumpa thamani mwenza wako kwa kumshirikisha mambo yako kwani ni muhimu sana labda kama uliyenaye si mtu sahihi kwako na ulimpata kimagumashi.
Kwa ushauri na maoni tembelea ukurasa wetu wa Mimi na Uhusiano kwenye Mtandao wa Kijamii wa Facebook, Ista:mimi_na_uhusiano au jiunge kwenye group letu la WhtsApp kwa namba iliyopo juu.