The House of Favourite Newspapers

Vita: Simba Walistahili

0

BAADA ya AS Vita kukubali kichapo cha bao 1-0 dhidi ya Simba, wachezaji wa timu hiyo wamesema kuwa Simba walistahili kushinda kutokana na walivyojitoa katika mchezo huo uliokuwa wa Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

 

Simba baada ya ushindi huo, ni kama imelipiza kisasi kutokana na kuwahi kufungwa mabao 5-0 katika msimu wa 2018/19 wakiwa ugenini katika Uwanja wa Des Martrys Pentecote lakini safari hii wamefanikiwa kushinda.

 

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, kiungo wa timu hiyo, Jeremy Mumbere, alisema Simba walistahili kupata ushindi kutokana na jinsi walivyocheza kwa kujituma tofauti na walivyocheza katika msimu wa 2018/19.

“Simba walijitoa haswa katika mchezo dhidi yetu, nakumbuka tulivyowafunga hapa 5-0, lakini safari hii wameshinda wao hii inatokana na wao kujituma zaidi.

 

“Kwa sasa Simba wana timu nzuri tofauti na awali, kwa upande wetu kupoteza hayakuwa matokeo mazuri ukizingatia tulikuwa nyumbani, naamini tutafanya vizuri katika michezo ijayo,” alisema Mumbere.

Naye kiungo mshambuliaji wa AS Vita, Amede Masasi, alisema kuwa hakutegemea wao kupoteza dhidi ya Simba kwani walijiandaa kushinda huku akiamini kuwa walipoteza mchezo huo dhidi ya timu bora.

 

“Tumepoteza mchezo wetu dhidi ya timu bora, sikutarajia ubora ambao walikuwa nao Simba hasa katika mchezo wa ugenini dhidi yetu, tutajipanga kwa michezo ijayo tufanye vizuri,” alisema kiungo huyo.

 

 MARCO MZUMBE, Dar es Salaam

Leave A Reply