MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo Desemba 1, 2017 amewaongoza wakazi wa Dar es Salaam katika maadhimisho ya siku ya UKIMWI duniani yaliyofanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijiji Dar.
Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Mhe. Samia amewaasa vijana kuacha kujihusisha na ngono zembe ili kuepuka kuendelea kuambukizwa ukimwi na kudhibiti maambukizi mapya ya ugonjwa huo hatari duniani kote.
Aidha, Makamu wa Rais amewataka akina dada wanaofanya biashara za kuuza miili yao kingono (machangudoa) kuacha mara moja kwani kufanya hivyo kutapelekea kupoteza nguvu kazi la kesho.
Kitaifa Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yanafanyika leo katika Mkoa wa Lindi ambapo Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa anawaongoza Watanzania wote katika katika maadhimisho hayo.
Wakati huohuo, Mkurugenzi wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Dkt. Albina Chuwa amesema:
“Utafiti wa mwaka 2016/17 umetoa viwango vya kufubazwa kwa virusi vya ukimwi (VVU) amabapo ni kama alama ya kuonyesha mafanikio ya matibabu. Watu wanaoishi na virusi hivyo wanaishi muda mrefu. Matatizo yanayotokana na hali hiyo yanapungua na ni mara chache kuwaambukiza watu wengine ambapo inaonyesha asilimia 52 ya watu wazima wenye umri wa miaka 15 na 16 virusi vyao vimefubazwa.
“Matokeo haya yanaonyesha kuwa misaada kutoka kwa wadau wa maendeleo ya kupambana na maambukizi ya ukimwi kama PEPFAR, Mfuko wa Dunia na programu nyingine, na wadau wengine ikiwemo serikali ya Tanzania, zina manufaa makubwa na mwenendo ni mzuri wa kufikia lengo la kitaifa la kuwa na angalau asilimia 73 ya watu ambao virusi vyao vya ukimwi vimefubazwa mpaka kufikia mwaka 2020.
NA DENIS MTIMA/GPL