The House of Favourite Newspapers

Vurugu Hotelini… Ebitoke Amponza Mlela!

KIKI imemtokea puani! Komediani na mwigizaji maarufu wa kike wa filamu za Kibongo asiyeishiwa vituko, Annastazia Exavery almaarufu kama Ebitoke, amempoza mwigizaji Yusuf Mlela, Amani limedokezwa.

 

Jumatatu ya Novemba 11, mwaka huu, Ebitoke alivamia mkutano wa waandishi wa habari ulioandaliwa na Mlela kwenye Hoteli ya Protea jijini Dar na kufanya vurugu zilizozua gumzo kila kona.

 

TUKIO LA KUTENGENEZA (KIKI)

Katika tukio hilo ambalo ni la kutengeneza (kiki) kwa asilimia mia moja, Ebitoke alifika mahali hapo na kwenda kumvua wigi mrembo aliyesemekana anatoka na Mlela aliyetajwa kwa jina la Beyonce na kumwacha akiwa na kipilipili kichwani, lakini lawama zote sasa zinaelekezwa kwa Mlela huku kukiwa na shinikizo la kuchukuliwa hatua.

EBITOKE ALIA KUSALITIWA

Kabla ya tukio hilo, siku chache zilizopita Ebitoke alilia mbele ya gazeti hili akilalamika kusalitiwa kimapenzi na kuchezewa na Mlela baada ya jamaa huyo kunaswa na Beyonce kwenye birthday ya mwigizaji Aunt Ezekiel, yapata wiki moja sasa.

 

“Nimeumia sana, roho inaniuma kumuona Mlela akiwa na mwanamke mwingine,” alisema Ebitoke alipoulizwa maoni yake baada ya Mlela kunaswa na Beyonce na kuongeza;

“Mlela ni tabia yake kuchezea wanawake, lakini sikubali, nitapambana mpaka dakika ya mwisho.”

 

MLELA MATUSI

Kufuatia tukio hilo, Mlela amejikuta akioga matusi kama yote na kuingia matatani kwenye vyombo mbalimbali vinavyosimamia sanaa kwa kumtumia Ebitoke kutengeneza kiki ya filamu yake mpya ambapo binti huyo alijikuta akibebwa msobemsobe na kwenda kutupwa nje na mabaunsa.

 

RUNGU LA BODI YA FILAMU

Kwa mujibu wa chanzo chetu cha kuaminika ndani ya Bodi ya Filamu Tanzania (BFT), chombo hicho lazima kitamchukulia hatua Mlela baada ya kufanya uchunguzi wake.

“Taarifa ambazo hatujazithibitisha ni kwamba mkutano huo wa waandishi wa habari uliandaliwa na Mlela, lakini juu ya kwamba tukio la vurugu ni la kutengeneza au kiki kama mitandao inavyosema, hilo lazima uchunguzi ufanyike ili kujiridhisha.

 

“Kama itabainika kwamba Mlela alidhamiria kumtumia Ebitoke kama ngazi ili kutengeneza kiki ya filamu yake mpya, hapo lazima kitamnukia Mlela,” kilisema chanzo hicho kikisisitiza kuwa hayo mambo ya kiki ndiyo yamesababisha kudorora kwa tasnia ya filamu nchini na kuongeza;

 

“Lakini ukiangalia ile video (ya vurugu ya Ebitoke) akivamia press conference (mkutano wa waandishi wa habari) nimewaona hawa ndugu zetu (wasanii) hili suala wamelipanga makusudi ili wapate kiki.

“Hivi hawa Bongo Movies kwa nini wasitumie nguvu zao kuhakikisha wanarudisha soko la filamu kwa kuwa wabunifu kuliko kupoteza muda kwa ajili ya kiki ambazo haziwasaidii?”

BODI YA FILAMU

Akizungumza na Gazeti la Amani kwa njia ya simu akiwa nchini Nigeria, Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Tanzania, Dk Kiagho Kilonzo ambaye alisema yupo safari, lakini mara tu atakaporejea nchini atalishughulikia tukio hilo.

 

“Acha nirudi kwanza nchini (Tanzania), halafu nipate mrejesho wa kile kilichotokea kwa maana ya nature ya tukio lenyewe, ndipo nitajua cha kufanya,” alisema Dk Kilonzo ambaye bodi yake iliyo chini ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ndiyo mlezi wa waigizaji nchini.

 

CHAMA CHA WAIGIZAJI

Kwa upande wake, Chama cha Waigizaji Wilaya ya Kinondoni, Dar kupitia kwa msemaji wake, Masoud Kaftany kilieleza kusudio lao la kukaa kikao ili kujua ni hatua gani zitachukuliwa.

“Tulikuwa busy na kuandaa Tamasha la Nyerere, lakini tumepanga kukaa kikao ili kujua kinagaubaga ni nini hasa kilitokea na ni hatua gani za kuchukua kwa sababu mambo haya yana impact (madhara) kubwa kwenye sanaa yetu,” alisema Kaftany.

 

MLELA ASHAMBULIWA KILA KONA

Kufuatia tukio hilo, mashabiki wa Ebitoke wamekuwa wakimshambulia Mlela kwamba amemtumia Ebitoke kimapenzi kisha kumdhalilisha.

Mmoja wa waliochukizwa na tukio hilo ni mwigizaji Esha Buhet ambaye alimshambulia Mlela kwa maneno makali mno.

 

“Wanaume mpoje lakini? Mbona kila siku kuumizana tu? Wewe si ulimleta huyo (Ebitoke) ukaniambia ndiye mwanamke wako? Haya maisha ya drama umeanza lini? Kwanza umri umeenda, tafuta mwanamke uoe, kazi kuumiza watoto wa wenzio, nimeumia sana, siyo sawa kabisa, upuuzi tu,” aliandika Esha mtandaoni akionekana kuchukizwa na sakata hilo bila kujali lilikuwa ni la kutengeneza au la kweli.

 

KWA NINI NI KIKI?

Kwa mujibu wa Meneja wa Hoteli ya Protea, Suleiman Victor alisema Mlela alifika hotelini hapo siku moja kabla ya tukio hilo kuweka ‘booking’ ya kufanya mkutano na waandishi na kati ya mambo aliyoambiwa na msanii huyo ni kwamba kuna mchezo wataufanya.

 

“Alikuja hapa hotelini na kutaka sehemu ya kufanya mkutano, lakini kati ya vitu alivyoniambia ni kwamba kuna drama wataifanya katika mkutano huo, japokuwa hakuniweka wazi ni nini wangefanya,” alisema Victor.

 

PENZI LA EBITOKE NA MLELA

Ebitoke na Mlela walianza mapenzi miezi miwili iliyopita, walikutana kambini visiwani Zanzibar wakati wa uzinduzi wa Swahiliflix kabla ya penzi lao kutumbukia nyongo wiki mbili zilizopita.

Comments are closed.