The House of Favourite Newspapers

Vyakula Hatari Na Vinavyofaa Kwa Wajawazito

0

WATAALAMU wa afya wanasema ili mwili ukue vizuri unahitaji vyakula vya aina tofauti tofauti. Iwapo una mtoto, mwili wake unahitaji virutubisho ili kusaidia ukuaji. Kama ni kijana mwili wake una mahitaji maalumu ili kukuza afya vizuri kuelekea utu uzima. Hii ni kwa sababu anapoelekea utu uzima anahitaji kuwa na uzito unaolingana na mwili wake. Kwa upande wa wajawazito na wanaonyonyesha nao wana vyakula vyao maalumu wanavyohitajika tofauti kabisa na wanawake wasio na mimba.

 

Uchunguzi mmoja uliofanywa kuhusu tiba unaonyesha kuwa, hali ya kiafya ya mjamzito huwa na athari mbalimbali kwa mtoto atakayezaliwa kama mama hatapata lishe bora. Si hivyo tu bali kuna ushahidi mkubwa kuwa magonjwa sugu ya watu wazima huanzia wakati mtoto akiwa bado tumboni mwa mama akiwa katika hali ya kiluilui au kitaalumu foetus.

 

Kwa hivyo, wajawazito wanashauriwa kuzingatia vyakula wanavyokula kabla na baada ya kushika mimba. Sasa tuangalie athari za chakula kwa afya ya mtoto na virutubisho vinavyopaswa kujumuishwa katika mlo wa mjamzito. Chakula cha mjamzito kinaweza kuwa na athari kubwa kwa afya ya watoto kwa miaka mingi baada ya kuzaliwa.

 

Miaka kadhaa ya hivi karibuni, Jarida la Masuala ya Lishe la Uingereza la Prestigious lilichapisha makala tatu kuhusu athari za lishe ya mama mjamzito kwa afya na ukuaji wa kiakili wa mtoto ambaye bado hajazaliwa. Wengi wanafahamu kuwa wajawazito wanapaswa kula chakula chenye virutubisho vyote vinavyohitajika ili kuhakikisha watoto wao watakaowazaa wamerutubika vya kutosha wakati wakiwa kwenye fuko la uzazi tumboni.

 

Hata hivyo, kile ambacho hatukubaliani nacho hivi sasa ni kwamba chakula cha mama mwenye mimba kinaweza kuwa na taathira (matokeo) chanya kwa afya ya watoto kwa muda wa miaka mingi, baada ya kuzaliwa mtoto.

 

Hivi sasa imethibitika kuwa kile kinacholiwa na akina mama wakati wa ujauzito, chakula ambacho kitakuwa kimejumuisha virutubisho vyote vinavyotakiwa, kama vile cha nafaka zisizokobolewa na matunda, kinaweza kuwafanya watoto wao watakaozaliwa kuwa werevu zaidi. Siku hizi unaweza kuandaa kizazi kipya cha watoto werevu kwa kula chakula kinachotakiwa wakati wa ujauzito.

 

Wajawazito ambao katika kipindi cha ujauzito hawakupata lishe bora isiyo na protini, nishati, madini na vitamini kwa ujumla huzaa watoto walio na uzito wa chini. Aidha, watoto hao huwa
na uwezekano mkubwa wa kupata magonjwa ya kisukari kipindi cha utu uzima.

 

MADHARA YA POMBE Baada ya kufahamu umuhimu wa kula lishe bora kwa mama mjamzito na athari zake chanya kwa mtoto atakayezaliwa, sasa tuangalie hatari ya unywaji pombe kwa wajawazito. Watu wengi wanafahamu madhara yanayotokana na utumiaji wa dawa za kulevya na dawa za kawaida pamoja na uvutaji sigara wakati wa ujauzito, lakini wanawake wengi hawana ufahamu wa kutosha kuhusu madhara yanayosababishwa nunywaji pombe wakati wa ujauzito.

 

Unywaji pombe wa aina zozote wakati mama akiwa na mimba huwa na madhara tofauti kwa mtoto aliye tumboni mwake, kuanzia zile za wastani hadi kubwa. Kuna madhara makuu matatu yanayoweza kumsibu mtoto ambaye bado hajazaliwa iwapo mama yake alikuwa akinywa pombe wakati wa ujauzito.

 

Mosi, ni kuweko hatari kubwa ya kutoka mimba au kuzaliwa mtoto kabla ya miezi tisa, pili, chembe za mwili za mtoto aliye tumboni zinaweza kuathiriwa au anaweza kuwa na uzito mdogo na kuzaliwa akiwa na ulemavu zaidi ya mmoja. Tatu, chembe za ubongo wa mtoto huyo zinaweza kuharibiwa na pombe na mtoto kuzaliwa akiwa na matatizo ambayo kitaalamu hujulikana kama foetal alcohol syndrome.

 

Miongoni mwa madhara yanayoweza kumpata mtoto ni kama vile kuzaliwa akiwa na ulemavu wa kimwili na kiakili. Kwa upande wa kimwili, mtoto huweza kuathiriwa na mtindio wa ubongo au brain retardation, mtoto anaweza kuzaliwa akiwa na kichwa kidogo sana, na uso wake kuwa na mwanya mkubwa baina ya pua na mdomo

Makala haya yameandikwa na Mtaalamu wa Lishe, Abdallah Mandai kwa ushauri piga 0717 961795, 0754 391 743.

Leave A Reply