Waarabu, TP Mazembe Kukipiga Simba Day
IPO wazi kwamba Septemba 19 mabingwa wa Ligi Kuu Bara, Simba kwenye Tamasha la Simba Day watacheza na moja ya vigogo wa Afrika kutokana na mabosi hao kuhitaji kucheza na timu ambayo imetwaa ubingwa wa Afrika zaidi ya mara tatu.
Upo uwekezekano wa Simba kucheza na Al Ahly ya Misri iliyochukua taji hilo mara tano, pia wapo TP Mazembe na Raja Casablanca waliochukua mara nne au karata itawangukia Wydad Casablanca ya Morocco iliyotwaa taji hilo mara tatu kama ilivyo kwa Esperance.
Akizungumza na Championi Jumamosi, Kaimu Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema: “Bado tunaangalia timu itakayotufaa lakini niwahakikishie kwamba tutacheza na timu ambayo imetwaa ubingwa zaidi ya mara tatu tena ule wa Afrika.“Kuelekea kwenye Simba Day tutatumia slogan ya ‘One Team, One Dream tukimaliza na Asubuhi Tu, Twendeni Wenye Nchi’. Pia kutakuwa na Wiki ya Simba ambayo itaanza Septemba 13 mpaka siku ya kilele Septemba 19.”
ISHU YA ANTONIO NUGAZ NA SALAMA JABIR
“Klabu ipo makini kwa namna inavyofanya. Mimi nilikuja Simba na hakukuwa na minong’ono popote, hivyo watu watulie tuone nani atatangazwa kuwa msemaji.”
JEZI MPYA UTATA
Jana, Simba ilizindua jezi mpya kwa msimu wa 2021/22 ambapo uzinduzi huo umekuja
ghafla baada ya awali kusema leo ndiyo zingezinduliwa.Kuzinduliwa mapema kwa jezi hizo kabla ya siku yake, kunatajwa ni baada ya kuvuja na kunaswa na ‘wahuni’ mitaani jambo ambalo wangezindua leo, kusingekuwa na jipya.
Baada ya kuzinduliwa kwa jezi hizo ambapo ilitangazwa zitauzwa maduka yote ya Vunja Bei ambao ndiyo watengenezaji na wasambazaji wakuu, mjadala mkubwa uliibuka, wapo waliosema ni nzuri kushinda zile za Yanga,
wengine wakasema wamekopi zile zilizotumiwa na Timu ya Taifa ya Tunisia kwenye AFCON 2019.
VIINGILIO SIMBA DAY
“Platinum Tsh 200,000 ambapo kutakuwa na chakula pamoja na usafiri kutoka sehemu watakayopata chakula,
jezi pamoja na kofia, VIP A Tsh 30,000, VIP B na C Tsh 2,000 na mzunguko ni Tsh. 5000.”
Waandishi: Lidia Kaaya, Maria Raymond, Hamisi Juma, Hawa Abouba