The House of Favourite Newspapers

Wageni walioiteka Marekani

0

Rihanna.

Hans Mloli na mtandao
WAHAMIAJI wapo kila mahali duniani lakini mara kadhaa huwa ni ngumu sana kung’ara au kuonyesha kipaji chako mbele ya wenyeji na kuwafunika kirahisi.

Drake.

Lakini wakati mwingine ishu ni kujiamini na kuendelea kupambana kama ilivyotokea kwa Rais wa Marekani, Barack Obama, ambaye baba yake ni Mkenya na sasa amefanikiwa kufungua njia na kutengeneza rekodi ya kuwa mtu mweusi wa kwanza mwenye asili kabisa ya Afrika Mashariki kulitawala taifa hilo gumzo zaidi duniani.

Ukiachana na hiyo, kwenye muziki wa nchi hiyo pia wageni kwa sasa wameshika usukani na ‘wanakimbiza’ kinoma. Inafika hatua inakuwa ngumu kutaja listi ya wasanii bora Marekani bila ya kuwepo ‘forena’ wawili au watatu.

Katika miaka ya hivi karibuni, Marekani imekuwa ikionekana kuwa na wasanii tishio dhidi ya mataifa mengine lakini ukitazama kwa undani zaidi, wengi wao walio juu wanaopeperusha bendera ya nchi hiyo katika masoko ya muziki duniani, hawatokei hapo na wengine hawana asili kabisa ya Marekani.

Rihanna

Nani asiyemfahamu Rihanna kwa sasa na kila mtu anamtaja kuwa ni Mmarekani, lakini huyu dada alizaliwa miaka 27 iliyopita kwenye mkoa mdogo wa St. Michael nchini Barbados.

Kipaji chake kilionekana akiwa na miaka 16, kilimuondoa nchini humo na kutua Marekani mikononi mwa Jay Z, kwa ajili ya kufanyiwa tathmini, akafaulu usahili na kusaini dili na kampuni kubwa ya lejendari huyo, Def Jam Recordings na kutoa ngoma yake ya kwanza, Pon De Replay iliyoshika namba mbili kwenye Billboard Hot 100.

Justin Bieber.

Kilichofuata baada ya hapo ilikuwa ni kutengeneza ngoma baada ya ngoma, pesa baada ya pesa, umaarufu uliokithiri na sasa ni moja kati ya wasanii wenye ushawishi na nguvu kubwa duniani.

Drake & Justin Bieber

Hawa wote walizaliwa Ontario nchini Canada, lakini kila mmoja alifika Marekani na ‘kutusua’ kimpango wake. Bieber alijulikana zaidi tangu awali kupitia matamasha mbalimbali ya kutafuta vipaji kabla ya kukutanishwa na Usher na kuzidi kumpa maujanja, dogo hakulaza damu akakazana na singo iliyomtambulisha zaidi duniani na kumuweka kwenye chati mpaka leo ni Baby aliyomshirikisha Ludacris iliyotoka mwaka 2010, akiwa na miaka 16.

Drake naye alianza harakati akiwa kwao na baadaye akajisogeza Marekani kwa ajili ya kucheki ‘michongo’ zaidi lakini mwaka 2009, milango ikafunguka baada ya kutoa ngoma mbili kali; Best I Ever Had na Successful, zilizoteka akili ya kiongozi wa Young Money Entertainment, Lil Wayne na kuamua kumpa mkataba kwenye lebo hiyo, tangu hapo ukawa mwanzo wa Drake usiokuwa na kikomo mpaka leo.

DJ Khaled

Jina lake kamili ni Khaled bin Abdul Khaled, huyu amezaliwa Marekani lakini asili yake ni nchini Palestina. Inaelezwa kuwa wazazi wake walihamia nchini humo kwa shughuli za kimuziki kabla ya kuzaliwa kwake.

DJ Khaled.

DJ Khaled awali hakuwaza kuimba lakini alipenda sana kuwa DJ na wazazi walimuunga mkono katika hilo ila baadaye katika harakati za kutaka kutusua, mwaka 1993 akakutana na Birdman na Pitbull. Safari ya muziki ikaanzia hapo na akafanikiwa kuliteka soko vilivyo mwaka 2006 kwa ngoma yake kali ya We Takin Over, aliowashirikisha kina Akon, T.I, Rick Ross, Birdman, Wayne na Fat Joe.

Tangu hapo Khaled amekuwa moto wa kuotea mbali na wengi wakivutiwa na staili yake ya ‘kupayuka’ kwenye nyimbo zake.

Nicki Minaj

Hiki ni kichwa kingine kinachosumbua duniani kwa kazi zake na kipaji chake, alizaliwa wilayani St. James katika Mji wa Port of Spain nchini Trinidad & Tobago. Baba yake ana asili ya Kihindi na mama yake ana asili ya Kiafrika.

Alihamia Marekani na wazazi wake akiwa na miaka mitano na alijiingiza kwenye muziki tangu mwaka 2007, baada ya kufeli kwenye maigizo lakini akahangaika kupata kampuni ya kuendeleza kipaji chake huku ‘akifosi’ kutoa nyimbo za hapa na pale.

Mwaka 2009, kwa mara nyingine Wayne akatumia fursa, akasaini dili na Nicki Minaj na sasa Nicki ni habari nyingine kwenye Hip Hop, amekuwa tishio mpaka kwa wanaume.

French Montana

Kama ilivyo kwa Khaled, kiuhalisia French ni Mwarabu aliyezaliwa Rabat, Morocco, lakini familia yake ilihamia Marekani akiwa na miaka 13. Kama ilivyo kwa wengine, French alitambua kipaji chake cha ku-rap mapema na akaanza kujishughulisha na muziki tangu mwaka 2002, kwa kurekodi katika CD ‘freestyle battle’ na washikaji zake na kuzisambaza sehemu mbalimbali.

Akapitia safari ndefu katika kutafuta jina lakini mwaka 2012, baada ya wengi kugundua kilichopo ndani yake, malejendari wakataka saini yake akiwemo Jay Z na Kanye West mmiliki wa Lebo ya GOOD Music.

Jamaa hakuwa na pupa na baadaye akajiunga na kampuni mbili za Bad Boy Records ya P Diddy na MMG ya Rick Ross na sasa amekuwa gumzo kila kona.

 

Leave A Reply