Wahitimu wa Akademi ya MultiChoice Watinga Bungeni
Wanafunzi wanne waliohitimu hivi karibuni mafunzo maalum ya uzalishaji filamu chini ya programu ya MultiChoice Talent Factory wamehudhuria kikao cha bunge la Tanzania kama wageni maalum wa Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo.
Katika ziara hiyo pia wanafunzi hao walikutana na wadau mbalimbali akiwemo naibu spika Dr. Tulia Akson waziri Dr. Harrison Mwakyembe, naibu waziri Juliana Shonza, naibu waziri Anthony Mavunde na katibu mkuu wa wizara Suzan Mlawi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na wahitimu hao katika viwanja vya bunge jijini Dodoma, viongozi hao waliwataka wahitimu hao kutumia mafunzo maalum waliyoyapata katika kuleta mapinduzi ya tasnia ya filamu hapa Tanzania.
Kwa pamoja wamekiri kuwa tasnia ya filamu ni moja ya tasnia zinazokuwa kwa haraka hapa nchini hivyo ni muhimu wanatasnia wawe na mafunzo ya kutosha na yanayoendana na wakati ili iweze kupambana na nchi nyingine katika soko la filamu ulimwenguni huku tukihakikisha kuwa kazi zetu zinaakisi mila, desturi, utamaduni na uzalendo wetu.
Akizungumza na wanafunzi hao baada ya kumtembelea ofisini kwake, Katibu Mkuu Suzan Mlawi amesisitiza ahadi ya serikali kushirikiana na wadau wa tasnia mbalimbali ili kuharakisha ukuaji wa tasnia hizo. Amesema ushirikiano kati ya serikali na wadau ni muhimu na kwamba serikali itaendelea kuhakikisha kuwa sera na kanuni zinaboreshwa ili kuakisi hali halisi ya ukuaji wa tasnia ya filamu.
Wanafunzi hao wanne – Wilson Nkya, Jane Moshi, Jamal Mohamed na Sarah Kimario wamehitimu mafunzo maalum ya mwaka mmoja yanayofadhiliwa na MultiChoice ambapo vijana 60 kutoka kote barani Afrika huchaguliwa kwa mafunzo hayo kutoka nchi mbalimbali. Programu hiyo ina vituo vitatu vya mafunzo ambapo kwa upande wa kusini mwa Afrika kipo Lusaka Zambia, kwa Afrika Mashariki na kati kipo Nairobi Kenya na kwa Afrika Magharibi Lagos Nigeria.
Awamu ya pili ya program hii itaanza mwezi Octoba 2019 ambapo wanafunzi wengine 60 watapata mafunzo hayo. Tanzania kwa mara nyingine tena itapeleka wanafunzi wanne.
Comments are closed.