WAKATI mfanyabiashara ambaye ni bilionea maarufu Bongo, Mohammed Dewji akisakwa kila kona bila mafanikio, kijana Christopher Stambuli (pichani) ambaye alitekwa siku 14, ameibukia kanisani na kuwaacha watu wamepigwa na butwaa.
Akitoa shukrani kwa Mungu na familia yake ndani ya Kanisa la Emmaus Bible Church Pentecostal lililopo Mbezi Luis, Dar, baba wa kijana huyo alieleza mkasa mzima wa kutekwa kwa siku 14. Alisema kwamba baada ya mwanaye kutekwa na watu wasiojulikana, alitoa taarifa polisi ambao walianza uchunguzi wao huku yeye na mke wake wakiwashirikisha wachungaji mbalimbali kwa ajili ya kumuombea kijana wao arudi.
Katika kuwashirikisha huko alifika katika kanisa hilo linaloongozwa na mchungaji wa mitume na manabii, Daud Mashimo ambaye alimweleza kwamba mwanaye ni kweli ni mateka lakini yupo salama hana tatizo lolote hivyo watamuomba Mungu na baada ya siku saba atarejea.
“Tuliomuomba Mungu na mchungaji na alituhakikishia atarudi baada ya siku saba baada ya maombi hayo, tuliamini japokuwa kama binadamu wakati mwingine tulikuwa tuna wasiwasi mkubwa.
“Kweli tulirudi hapa kanisani kwake siku ya saba tukaomba pamoja na waumini na mchungaji akasema siku hiyo kijana atarejea, kweli ilipofika saa mbili usiku nilipata meseji ikisema kwamba yupo hospitali baada ya kuachwa na watu wasiojulikana maeneo ya stendi ya Mwenge,” alisema Stambuli.
Akizungumza kijana Christopher alisema anamshukuru Mungu amerudi salama ila kutokana na kwamba suala hilo polisi wanaendelea na uchunguzi ili kubaini waliohusika haruhusiwi kueleza ilikuwaje mpaka akawa mateka ni mpaka hapo baadaye wahusika watakapopatikana. Kijana huyo alikiri kutekwa akiwa maeneo ya Mwenge jijini Dar na kupelekwa kusikojulikana kwa kuwa alikuwa amefungwa kitambaa cheusi usoni. Alichokuwa akifanya/kufanyiwa akiwa huko alisema hawezi kuongea kwani suala lake bado liko polisi.
KANISA LAZIZIMA
Kutokana na ushuhuda huo, kanisa lilizizima kwa vifijo na vigelegele kwa waumini kushangilia na kumshukuru Mungu kwa jambo kubwa alilotenda kwa kijana huyo kwani wengi hutekwa lakini hawarudi.
MO AANGUSHIWA MAOMBI
Pamoja na kijana huyo kuibukia kanisani hapo, mchungaji Mashimo aliwaongoza waumini katika maombi maalum ya kumuombea MO ili aweze kupatikana kwani naye hajulikani alipo. Akieleza mchungaji huyo alisema kuwa MO yupo salama na atapatikana akiwa mzima japokuwa afya yake ndiyo itakuwa imedhoofu kiasi.
“Mungu alinionyesha kwamba MO atapatikana Oktoba 12, lakini hakuonekana kwa sababu kuna watu walichinja mbuzi wawili kwa ajili ka ajili ya kuomba arudi lakini Mungu akanionesha tena akasema ataonekana baada ya siku chache ili utukufu wake ujidhihirishe kwa watu wote duniani. “Kwa Mungu wetu hakuna kuchagua dini wala kabila, anaangalia uhitaji wa watu wake hivyo basi nawahakikishia Watanzania na dunia nzima kwamba MO atapatikana akiwa mzima,” alisema Mchungaji Mashimo.
TUJIKUMBUSHE
Oktoba 11, mwaka huu mfanyabiashara MO ambaye pia ni mwekezaji wa Klabu ya Simba, akielekea kwenye mazoezi ya viungo ‘gym’ katika Hoteli ya Colosseum, Oysterbay jijini Dar alitekwa na watu wasiojulikana na mpaka sasa anasakwa ili ijulikane alipo.
Stori: GLADNESS MALLYA, Dar
Comments are closed.