The House of Favourite Newspapers

Wala Sio Makonda; Aliyeleta Balaa Hili la Madawa ya Kulevya ni Huyu

Pablo Emilio Escober Gaviria

Na ELVAN STAMBULI| GAZETI LA UWAZI| NIJUAVYO MIMI

KILA kona hivi sasa katika nchi yetu, mjadala mkubwa ni vita dhidi ya madawa ya kulevya. Ni vita aliyoianzisha Mkuu wa Mkoa wa Dar, Paul Makonda lakini sasa imesambaa nchi nzima na duniani pia, ni kama moto wa kiangazi kwenye pori lenye majani makavu.

Nani amesababisha madawa haya kusambaa dunia nzima? Nionavyo mimi leo niwaletee mtu aliyechangia sana dunia kutikisika kutokana na madawa ya kulevya, msome mtu huyo hapa.

Katika milima inayotazamana na mji wa Medellín nchini Colombia, yapo majengo ya kifahari ndani ya milima hiyo ambayo sasa yanatumika kama nyumba ya watawa wa Kanisa Katoliki lakini kabla ya watawa hawa kupewa mwaka 2007, majengo haya yalikuwa ni gereza ambalo lilijengwa mwaka 1991 kumuhifadhi mfungwa maalumu raia wa Colombia.

Gereza hili licha ya kuwa mali ya serikali lakini michoro yake ilichorwa na kubuniwa na mfungwa mwenyewe na hata askari magereza ambao walikuwa wanalinda gereza hili walichaguliwa na mfungwa mwenyewe na hata polisi wa nchi ya Colombia walikuwa hawaruhusiwi kusogelea gereza hilo hata umbali wa maili 12.

Kwenye gereza hilo pia kulikuwa na chumba maalumu cha michezo ya watoto maalumu kwa ajili ya watoto wa mfungwa huyo pindi akitembelewa na familia yake. Na pia ndani ya gereza kuliwekwa darubini (Telescope) ya kumuwezesha mfungwa huyo kuangalia katika mji wa Medellín ambako familia yake iliishi na kila siku jioni alitoka nje kibarazani kuongea naye kwenye simu huku akiwatazama kwa darubini hiyo.

Gereza hili lilijulikana kama La Catedral (The Cathedral) na lilimuhifadhi mfungwa huyo ninayemzungumzia aliyesababisha biashara ya mihadarati iwe jinsi ilivyo hivi leo duniani, mtu huyo ni Pablo Emilio Escober Gaviria au kwa kifupi Pablo Escobar kama ulimwengu ulivyomtambua.

Akiwa bado kwenye umri mdogo, Pablo mara kwa mara aliwaambia ndugu na marafiki zake kuwa anataka awe na utajiri wa kiasi cha pesa milioni moja za Colombia atakapofikisha umri wa miaka 22.

Ndoto hizi zilimfanya ashindwe kumaliza chuo kikuu alipokuwa anasoma Universidad Autónoma Latino Americana of Madellín na kujiingiza katika biashara za halali na haramu na hatimaye aliacha masomo chuoni. Moja ya biashara zake haramu za kwanza kabisa akiwa kijana chini ya miaka 21 ilikuwa ni kutengeneza vyeti bandia vya stashahada vya chuo alichokuwa anasoma na kuwauzia watu waliohitaji kwa ajili ya kwenda kupata ajira.

Muonekano wa Jengo la Pablo huko Madellín

Pamoja na biashara hiyo pia Pablo alijihusisha na kusambaza mizigo ya sigara zilizokuwa haziruhusiwi nchini Colombia (Marlboro), akawa mhalifu. Kutokana na uzoefu wake wa ulimwengu wa kihalifu, Pablo aligundua kuwa zao la coca linalimwa nchini Bolivia ambalo linatumika kutengeneza Cocaine ni bora zaidi kuliko Coca inayolimwa nchini kwake Colombia.

Hivyo basi, Pablo akadhamiria kuwa kama anaingia kwenye biashara hii ya kusafirisha Cocaine ni lazima mihadarati yake iwe tofauti na bora zaidi kuliko Cocaine nyingine watu waliyozoea kutumia.

Akadhamiria kufanya Cocaine yake iwe daraja la kwanza ili kuvutia watumiaji na kufanya soko likue kwa haraka. Mwaka 1975 Pablo alisafiri mpaka nchini Bolivia kukutana na Roberto Suaréz Goméz ambaye marafiki zake walipenda kumuita El Padrino (The Godfather), kiongozi wa genge lililoitwa La Corparacíon (The Corporation).

Pablo alimpata na kumpa wazo Suaréz kuwa atumie ushawishi wake alionao serikalini akutane na kiongozi wa Cuba, Fidel Castro ili wamuombe aruhusu ndege zao za mizigo zitue kwenye viwanja vya ndege vya Cuba na kujaza mafuta, Castro aliwakubalia kwa sharti la  mihadarati hiyo isiuzwe ndani ya Amerika ya Kusini bali isafirishwe na kuuzwa Marekani ambapo alisisitiza kuwa atafurahi akiona vijana wa mabepari wakiharibika akili kwa mihadarati.

Baada ya Cocaine ya Pablo kuingia kwenye soko Marekani uhitaji na biashara ya mihadarati ya Cocaine ilipaa kwa kasi ya ajabu na Pablo Escobar akaanzisha rasmi genge lake la biashara ya mihadarati na akaliita Medellíne Cartel. Ili kufanikisha usafirishaji wa mihadarati yake kwa ufasaha na uhakika, Pablo alinunua ndege za mizigo 15 za ukubwa wa kati na helikopta sita.

Pablo

Pia alinunua nyambizi (submarines) ndogo. Hadi kufikia mwaka 1985 Pablo alikuwa anasafirisha takriban tani 70 mpaka 80 za Cocaine kwa mwezi na alikuwa ameshikilia asilimia 80 ya soko la mihadarati la Marekani. Katika miaka ya 1990 utajiri wake ulifikia Dola za Kimarekani bilioni 30 na Jarida maarufu la Forbes lilimuorodhesha Pablo Escobar kama mtu namba tano tajiri zaidi duniani.

Moja ya vitu muhimu vya kihalifu alivyovifanya Pablo na kufanikiwa kuibuka kinara wa uhalifu Amerika ya Kusini ilikuwa ni kutekeleza sera yake aliyoianzisha ili kuidhibiti serikali na vyombo vya ulinzi ambapo sera hii aliita “Plata o Plomo”  (fedha au risasi)). Akiwa na maana kwamba kama wewe ni mtu wa serikali na ikitokea mmesigana basi atakupa fedha (rushwa) kama ukikataa kupokea basi anakupiga risasi kwa kutumia watu wake.

Aliwahi kukamatwa na alitoroka jela akawa anatafutwa. Baada ya mwaka mzima wa msako mkali hatimaye Desemba 2, 1993 jeshi la Colombia lilifanikiwa kunasa mawasiliano ya simu kati ya Pablo na wasaidizi wake.

Wakatumia ‘triangulation technology’ kung’amua mahali alipo katika Mtaa wa Los Olivos katika mji wa Madellín. Baada ya kufanikiwa kufahamu nyumba aliyojihifadhi pasipo kupoteza muda wakafanya shambulio la kushitukiza. Mlinzi wa Pablo alipigwa risasi na kufariki papo hapo na Pablo alipigwa risasi mguuni na akajikongoja mpaka juu ya paa.

Wanajeshi waliingia ndani walipanda juu ya paa na walimkuta Pablo amelala chini amefariki dunia akiwa na tundu la risasi aliyopigwa kwenye sikio na kutokea upande wa pili wa kichwa.

Marafiki zake wa karibu pamoja na kaka yake wa kuzaliwa wanasema kwamba siku zote Pablo alikuwa anasema kuwa hatakubali kupigwa risasi ya mwisho na adui yake, kama ikitokea ameshambuliwa na adui na hana namna ya kujiokoa basi atajipiga risasi sikioni itokee upande wa pili.

Huo ndiyo ulikuwa mwisho wa Pablo katika dunia hii kwa kifupi sana,  ndiye aliyesababisha leo Makonda afanye anayoyafanya katika Dar yake mpya dhidi ya madawa ya kulevya.]

Hapa tumekuanikia kurasa za mbele na za nyuma za magazeti yote ya Tanzania leo, Februari 28, 2017. Ni yale ya Hardnews, Udaku na Michezo.

Kwa stori zote kali, Tu-follow

Facebook @Globalpublishers

Twitter @GlobalHabari

Instagram @GlobalPublishers

YouTube @GlobalTVTZ

Shinda Nyumba Awamu ya Pili Yatikisa Jiji la Dar es Salaam

Comments are closed.