The House of Favourite Newspapers

Walioishi ardhini siku 41 simulizi yao inatisha

0

JOSEPH BURURE akiwa na kaka yake Michael BurureMmoja wa wahanga hao akiwa hospitali.


Na Idd Mumba, KAHAMA

MWACHENI Mungu aitwe Mungu! Ndiyo lugha ya pekee inayoweza kutumika katika maajabu yake ya uumbaji aliowafanyia Watanzania watano waliofukiwa na kifusi mgodini na kujikuta wakiishi humo kwa siku 41 mpaka kuja kuokolewa wakiwa hai.

Almanusura hao ni Joseph Burure (42), mkazi wa Wilaya ya Tarime Mara, Amos Hangwa (25), mkazi wa Kwimba, Mwanza, Msafiri Gerald (38), mkazi wa Sumbawanga Rukwa, Chacha Wambura (54), mkazi wa Mara na Onyiwa Kado (55), mkazi wa Tarime ambaye amefariki dunia juzi.

Kuna kila sababu ya kumshukuru Mungu kwa kila jambo ambalo anawajalia wanadamu maishani mwao kila siku! Sasa ni takriban siku kumi zimekatika tangu kutokea kwa tukio hilo ambalo limekuwa gumzo kwenye vyombo vya habari na kuibua hisia za hali ya juu kwa wengi, wakisema ‘kweli Mungu ni mkubwa na njia zake hazichunguziki’.

Baada ya kupata taarifa za almanusura hao, Gazeti la Uwazi kama ilivyo kawaida yake, lilifunga safari mpaka kwenye Mgodi wa Dhahabu wa Shigito uliopo katika Kijiji cha Nyangarata Kakola wilayani Kahama, Shinyanga na Hospitali ya Wilaya ya Kahama ambako watu hao wamelazwa.

Lengo la Uwazi ni kuchimba kwa kina tukio hilo ambalo limeishangaza dunia na kumjua Mungu kwa undani zaidi.

OKTOBA 5, 2015
Kwa mujibu wa mchimbaji mmoja aliyenusurika aitwaye Paschal, siku hiyo ya kifusi kutitia na kufunika wachimbaji, ilikuwa saa mbili asubuhi ya Oktoba 5, mwaka huu. Wachimbaji wa mgodi huo 21 waliingia kwenye shimo lao la kufanyia kazi.

“Sasa tukiwa tunaendelea kuchimba, ghafla tukasikia kishindo kikuu na giza kuzidi kuwa kubwa kama vile kuna watu walituwekea mikono kwenye macho ili tusione chochote.

“Mimi na wenzangu kumi tukatoka kupitia mlango mwingine. Kufika nje tukakuta taharuki, wachimbaji waliokuwa juu wakikimbia huku na kule wakisema tulioingia mgodini tumefukiwa na kifusi kwani udongo juu umetitia na shimo la kuingilia limeziba.

WAJIHESABU
“Sisi tuliotoka tulijihesabu na kubaini ni kumi na moja. Ndipo jitihada zikaanza palepale ili kuwaokoa wenzetu kumi ili kukamilisha hesabu ya watu 21. Ni kawaida mkiingia mgodini lazima hesabu ijulikane ni watu wangapi wameingia na kutoka!

WANNE WAOKOLEWA
“Basi, kazi ilikuwa ngumu kidogo tukisaidiwa na watu wa serikali, tukafanikiwa kuwaokoa wengine wanne. Wakabaki wenzetu sita ambao ilionekana hakuna namna ya kuwakoa kutokana na uhaba wa vifaa licha ya jitihada za serikali kuhakikisha watu hao wanatolewa wakiwa hai au wamepoteza maisha. Hawa sita walishindwa kutoka kutokana na mlango wa kutokea juu kuzibwa na kifusi kilichokuwa kimedondokea shimoni.

OKTOBA 6, 2015
Mchimbaji huyo alisema waokoaji waliendelea na juhududi za kuokoa maisha ya watu waliokuwa wamefukiwa na kifusi katika mgodi huo ambapo walifanya kazi hiyo usiku na mchana kuhakikisha wananusuru maisha ya wenzao lakini mambo yalikwama kwa takribani siku tatu.

OKTOBA 9, 2015
Oktoba 9, mwaka huu, Serikali ya Kijiji cha Nyangarata Kakola ikaomba msaada wa vifaa na uokoaji kutoka Mgodi wa Acacia ili kufanya kazi hiyo lakini ikashindikana baada ya wataalam wa mgodi huo kusema kuwa, uwezekano wa kuwaokoa watu hao wakiwa hai ni mgumu kutokana na mazingira yalivyo pamoja na namna kifusi hicho kilivyoanguka hivyo waliwataka wachimbaji wa mgodi huo kuwasiliana na serikali kuu ili iwapatie mafuta ya kutumia kuokoa miili ya marehemu.

kaka

Akipata matibabu.

SERIKALI YATOA LITA 7,500 KUSAIDIA, WAJANJA WAZICHAKACHUA
Naye mwenyekiti wa bodi ya mgodi huo, Hamza Tandiko alisema tangu tukio hili litokee wamekuwa pamoja na serikali kwa kila hatua kuhakikisha maisha ya ndugu hao yanaokolewa.

Alisema: “Naibu Waziri wa Nishati na Madini (wakati huo), Charles Mwijage alitoa lita 7,500 ili ziweze kutumika katika uokoaji kwa kutumia vifaa vya Mgodi wa Acacia lakini mpaka zinapita siku zote hizo hakuna kitu kilichofanyika.

“Hata hayo mafuta hatujayaona, sijui yalikwenda wapi kwani yangetumika kama ilivyokuwa imeagizwa nadhani tungewaokoa wote wakiwa hai.”

SIKU 15 ZAKATIKA
Siku15 zilikatika tangu wachimbaji sita kuwa ardhini na jitihada za kuwakoa kushindikana, mchimbaji mwingine alijaribu kuingia katika mgodi huo kwa lengo la kuokoa baadhi ya mashine zilizokuwa zimefukiwa na kifusi hicho ambapo katika hali asiyoitarajia, alisikia sauti za watu zikitaka msaada hivyo alipotoka alitoa taarifa kwa viongozi ambao walikwenda kuwaarifu polisi.

POLISI WAFANYA TUKIO LA AJABU
“Lakini cha ajabu, hatua hiyo haikupokelewa vizuri na jeshi la polisi kwani walimkamata mtoa taarifa huyo na kumweka ndani bila kufanya uchuguzi wa undani wa taarifa hiyo. Wao wakamfanya mtoa taarifa huyo kuwa mtuhumiwa bila sababu yoyote,” alisema mchimbaji huyo aliyenusurika.

MAZISHI YA KIMILA, WAOMBOLEZA
Baada ya taarifa hiyo kushindwa kufanyiwa kazi na polisi kama ilivyotolewa, wachimbaji waliendelea kufanya shughuli zao katika mashimo mengine huku ndugu, jamaa na marafiki wa waliokuwa ardhini wakifanya mikusanyiko ya kuomboleza na kufanya mazishi ya kimila kutokana na ndugu hao kutopatikana miili.

Kwa vile, wengi wa watu hao ni Wakurya, hivyo kwa mila na desturi zao, ndugu walichukua mchanga na mawe ya eneo husika na kwenda kuzika makwao, mkoani Mara.

mwandishi wa habari hii idd mumba akifanya mahojiano Msafiri Geradi (38) alipowatembelea katika hospitali ya wilaya ya kahamaMUNGU MKUBWA!!!
Kweli Mungu mkubwa! Baada ya siku nyingi kupita tangu kutokea kwa tukio hilo la kutisha, kuna mashine ambazo zilitumika kusambaza maji na chakula kwa wachimbaji nazo zilifukiwa na kifusi hicho, hivyo mmiliki wa mashine hizo aliahidi kutoa fedha kiasi cha shilingi laki tano (500,000) kwa mchimbaji yeyote atakayefanikiwa kuzitoa mashine hizo katika shimo la mgodi huo lililokuwa limefukia watu sita.

Walijitokeza vijana wawili na kuahidi kuifanya kazi hiyo kwa kuingia shimoni kwa namna wanavyojua wao. Uwazi lilizungumza na vijana hao ambao ni Mussa Rashid Binde (27), mkazi wa Kondoa na Lucas Labloo (26), mkazi wa Manyara.

Msikie Mussa: “Basi baada ya ofa hiyo, sisi tulishuka chini mgodini kwa umbali wa kama mita 112 hivi, tukasikia sauti za watu zikitaka msaada. Tulishtuka sana na kuamua kutoka nje ambapo hatukutoa taarifa kwanza. Tulikaa wenyewe tukijadiliana tufanye nini! Tulipata wazo la pamoja la kurudi tena ndani ya shimo ili kujiridhisha kama kweli zile ni sauti za watu au majini.

“Tulipozama tena umbali uleule tukasikia sauti zikisema; ‘jamani hatujafa, tuko hai.’ Tulizitambua sauti hizo ikabidi tuite majina ya wale waliofukiwa kama ndiyo wenyewe. Mimi nilimwita Joseph, akaitika, nikarudia mara tatu, naye akaniita Mussa. Ndipo tukatoka nje kwenda kutoa taarifa kwa uongozi wa mgodi.”

Kutokana na ufinyu wa nafasi, simulizi hii ya kutisha itaendelea wiki ijayo kwenye gazeti hilihili ambapo utajua namna watu hao walivyookelewa na pia utawasikia wenyewe wakisimulia kwa mapana maisha yao ndani ya ardhi yenye giza nene kwa siku hizo 41.

Leave A Reply