The House of Favourite Newspapers

Waliokuwa Maofisa wa TanTrade Wahukumiwa Miaka 3 Jela

0
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imewahukumu kwenda jela miaka mitatu au kulipa faini ya Sh5 milioni kwa kila kosa waliokuwa Mkurugenzi wa Utafiti na Mipango wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (Tan Trade) Samweli Mvingira na Naibu Mkurugenzi wa Fedha na Utawala,  Judith Msuya baada ya kupatikana na hatia ya kutumia madaraka yao vibaya na kuisababishia Serikali hasara.
Hata hivyo, mshtakiwa Judith Msuya ambaye alikuwa ni Naibu Mkurugenzi wa Fedha na Utawala kutoka Mamlaka hiyo (Tan Trade) amelipa faini hiyo na kuepuka kifungo cha miaka mitatu jela.
Washtakiwa kwa pamoja wametiwa hatiani katika mashtaka manne kati ya matano walioshtakiwa nayo mahakamani hapo  likiwemo la kutumia madaraka yao vibaya kwa kuagiza gari lililotumika kinyume cha Sheria ya Manunuzi ya Umma iliyosababisha AL Hamadi Motors FZD kupata faida ya Sh34. 89 milioni.
Katika kesi hiyo, washtakiwa walikuwa watatu akiwemo aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Tan Trade ambaye alifariki dunia wakati shahidi wa kwanza alipotoa ushahidi wake.
Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mkazi Mfawidhi, Cyprian Mkeha amesema ameridhishwa na mashahidi wa upande wa Jamhuri ambao wameweza kuthibitisha mashtaka dhidi ya washtakiwa hao.
“Nimewatia hatiani washtakiwa  hawa kwa makosa manne ya kutumia madaraka vibaya, hivyo kosa la kwanza hadi la nne mtalipa faini ya Sh 5milioni kwa kila kosa au kwenda jela miaka mitatu kwa kila kosa na shtaka la tano nawaachia huru kwa sababu Jamhuri imeshindwa kuthibitisha shtaka hili,” amesema Hakimu Mkeha.
Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, washtakiwa wanadaiwa kuwa kati ya Septemba 2007 na Julai 2008, Makao Makuu ya TanTrade wilaya ya Temeke walitumia madaraka yao vibaya kwa kuagiza gari lililotumika kinyume cha Sheria ya Manunuzi ya Umma iliyosababisha AL Hamadi Motors FZD kupata faida ya Sh34.89 milioni.
Katika shtaka la pili, tarehe hiyo na mahali hapo, washtakiwa kwa kutumia madaraka yao vibaya, walinunua gari iliyotumika kwa lengo la kumnufaisha Humer Stars kiasi cha Sh32.77 milioni.
Katika shtaka la tatu, washtakiwa wanadaiwa bila kufuata utaratibu wa kushindanisha zabuni waliagiza gari iliyotumika na kusababisha AL Hamad kupata faida ya Sh34.89 milioni huku shtaka la nne watuhumiwa walinunua gari bila kufuata utaratibu wa zabuni.
Shtaka la tano, ambalo washtakiwa waliachiwa huru baada ya Jamhuri kushindwa kuthibitisha shtaka, washtakiwa walidaiwa kutumia madaraka yao vibaya, uzembe na kumsababishia mwajiri wao hasara ya Sh49.145 milioni.
Leave A Reply