Waliouawa na Kujeruhiwa Mgodi wa Mwadui Kulipwa Mamilioni
HATIMAYE Kampuni ya Petra Diamonds ya nchini Uingereza inayomiliki mgodi wa almasi wa Williamson uliopo Mwadui, Shinyanga imekubali kulipa fidia ya dola milioni sita za Kimarekani kwa wachimbaji 71 wa Kitanzania ambao haki zao za kibinadamu zilivunjwa na mgodi huo.
Katika taarifa iliyotolewa na uongozi wa kampuni hiyo, watakaolipwa ni wachimbaji waliovamia mgodi huo na kuendesha uchimbaji haramu ambapo wengine waliuawa, kupigwa na kusababishiwa ulemavu na kunyanyaswa na walinzi wa mgodi huo.
Uchunguzi wa matukio hayo ya kuvunjwa kwa haki za binadamu za wachimbaji kwenye mgodi huo ulianzishwa miaka kadhaa iliyopita na shirika lisilo la kiserikali la Rights and Accountability in Development (Raid) la nchini Uingereza ambapo waathirika wa matukio hayo waliwakilishwa kwenye kesi hiyo na wanasheria wa haki za binadamu kutoka Kampuni ya Leigh Day.