The House of Favourite Newspapers

Walishikwa Wasanii Hawa… Wakatoboa Mkono

BILA shaka utakuwa unafahamu majina makubwa ya wasanii wa Muziki wa Bongo Fleva kwa sasa. Kitu ambacho unaweza usikifahamu ni namna gani wasanii hao walitoboa katika gemu yao ya muziki.

Leo katika Mikito Nusunusu nimekuletea listi ya baadhi tu ya mastaa wanaotamba kwenye muziki huo Bongo, ambao walishikwa mkono na mastaa wakubwa wakatoboa.

DOGO JANJA

Mama yake mzazi anapenda kumuita Abdulaziz Abubakar Chende lakini yeye mwenyewe amechagua jina la kutafutia ‘ugali’ kama Dogo Janja ama Janjaro.

Dogo Janja alianza rasmi kufanya Muziki wa Hip Hop Bongo mwaka 2009 baada ya kushikwa mkono na msanii Madee Ali alipokwenda kwenye shoo moja jijini Arusha na kuamua kumchukua.

 

Tangu hapo, Janjaro alianza kufahamika na kujizolea umaarufu ndani na nje ya Bongo na mpaka leo hii bado yupo chini ya lebo ya Madee iitwayo Manzese Music Baby (MMB) akiwa ameshado

ndosha ngoma za kutosha kama vile My Life, Anajua, Banana, Wayu Wayu, Ngarenaro, Ukivaaje Unapendeza na nyingine kibao.

BILLNASS

Ukiweka kando kizungumkuti cha uhusiano na msanii mwenzake, Faustina Charles ‘Nandy’, moto wa rapa William Lyimo ‘Billnass’ umekuwa wakuotea mbali tokea alipoingia kwenye gemu ya Hip Hop Bongo.

 

Unajua alitokea wapi? Billnass ama Nenga kama anavyopenda kujiita, alishikwa mkono na lejendari TID baada ya kumtambulisha kwenye gemu kupitia kolabo ya Ligi Ndogo huku akimsimamia kupitia lebo yake ya Rada Entertainment.

 

Hawakudumu sana, Billnass aliondoka kwenye lebo hiyo na kuanzisha lebo yake ya LFLG na kufanikiwa kuachia ngoma ‘hits’ kama Chafu Pozi, Tagi Ubavu, Funga Geti, Sina Jambo, Kwa Leo, Mazoea, Raha na Bugana inayokimbiza kwa sasa.

HARMONIZE

Waliosoma naye huko Chitoholi, Mtwara wanamtambua sana kwa jina la Abdulkhali Rajab lakini baada ya kutua Bongo ndani ya Lebo ya WCB, jina lilibadilika na kuwa Harmonize ama Konde Boy.

Umaarufu wake na mafanikio ndani ya muda mchache umewavutia vijana wengi kutokukata tamaa kwenye maisha.

 

Tangu mkali huyu ashikwe mkono na Diamond Platnumz chini ya WCB na kuachia Ngoma ya Aiyola mwaka 2015, ameweza kuwa moja kati ya wasanii wenye majina makubwa ndani na nje ya Bongo mpaka kufikia hatua ya kushindanishwa na baba yake kimuziki, Diamond Platnumz.

Kwa sasa Harmonize mwenye ngoma kibwena kama Never Give Up, Kainama, Bado, Kwangwaru, Niteke, Atarudi, Paranawe na Zilipendwa, anadaiwa kujitoa WCB na kuanzisha lebo yake ya Konde Gang.

MALAIKA

Diana Exavery Clavery a.k.a Malaika alianza kutikisa Bongo kwa sauti yake ya kipekee baada ya kushirikishwa kwenye kolabo na mkali Chege Chigunda kupitia Ngoma ya Uswazi Take Away.

Awali hakuwa akiamini katika kutoka kimuziki. Ndiyo kwanza alikuwa akiwafanyia wasanii make up katika Studio za Visual Lab chini ya Adam Juma.

 

Mara nyingi Malaika amekuwa akinukuliwa kutoa maneno mazuri ya kumshukuru Chege Chigunda kwa kuamini katika kipaji chake na kumpa nafasi.

Licha ya kukaa muda mrefu bila kutoa wimbo, bado mrembo huyo anatikisa mitaa na hits zake kama Saresare na Rarua zinazotoboa spika kwenye sherehe za watu mbalimbali.

RAYVANNY, MBOSSO NA LAVA LAVA

Hawa wote ni zao la Lebo ya WCB baada ya kushikwa mkono na Diamond Platnumz ambaye ndiye mmiliki wa lebo hiyo.

 

Diamond aliamini katika vipaji vya vijana hawa na kuamua kuwainua katika tasnia ya muziki, jambo ambalo limezaa matunda, kwani wamedhihirisha hilo kwa kazi zao nzuri zinazokubalika kila kona.

 

Ikumbukwe kuwa Rayvanny alitokea Lebo ya Tip Top Connection na Mbosso alitokea Lebo ya Mkubwa na Wanawe chini ya Mkubwa Fella lakini tangu watue WCB mafanikio yao yamekuwa makubwa zaidi.

MAKALA: JULIUS ZOMBA

Comments are closed.