The House of Favourite Newspapers

Wanajeshi wa UN Wagundua miili 50 ndani ya Makaburi Mawili Mashariki mwa DRC

0

Wanajeshi wa Umoja wa mataifa wamegundua miili 50 ya raia ndani ya makaburi yaliyozikwa watu wengi kwa pamoja mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, maafisa wamesema. Hayo yamejiri baada ya msururu wa mashambulizi yanayodaiwa kufanywa na makundi yenye silaha.

Wanajeshi hao wa Umoja wa mataifa waligundua miili hiyo wakati wakipiga doria katika jimbo lenye machafuko la Ituri kufuatia mashambulizi mabaya yaliyofanywa na wanamgambo wanaodhaniwa kuwa wa kundi la CODECO.

“Wenzetu kule wameripoti kwamba kaburi la pamoja lenye miili 42, wakiwemo wanawake 12 na watoto 6 limegunduliwa katika kijiji cha Nyamamba,” amesema naibu msemaji wa Umoja wa mataifa Farhan Haq.

Ameongeza kuwa kaburi nyingine ikiwa na miili 7 iligunduliwa katika kijiji cha Mbogi.”

Haq ameomba kufanyike uchunguzi ambao utabaini ikiwa kuna uhusiano kati ya makaburi hayo na mashambulizi ya wanamgambo hao.

“MONUSO inaunga mkono mahakama za Congo kuchunguza mashambulizi hayo na kuwafikisha wahusika mbele ya vyombo vya sheria,” Haq amesema.

Ituri, jimbo linalopakana na Uganda, limeshuhudia machafuko katika wiki za hivi karibuni, baada ya mauaji ya mwalimu mmoja kutoka jamii ya Walendu kuchochea mashambulizi ya ulipizaji kisasi yaliyofanywa na kundi la wanamgambo la CODECO, ambalo linadai kuwakilisha Walendu.

Leave A Reply