WAKATI mchakamchaka wa kampeni ukiendelea kupamba moto katika maeneo mbalimbali huku wagombea urais, ubunge na udiwani wakinadi sera zao ili wachaguliwe na wananchi kuwaongoza katika uchaguzi Mkuu wa Oktoba 28, 2020, Jimbo la Buchosa nako mambo yamenoga.
Wananchi wa vijiji mbalimbali vya jimbo hilo wamejitokeza kuchukua jarida maalum lenye mambo mazito ndani yake ambayo mgombea ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Eric Shigongo James, anayaahidi kuyafanya endapo watampa ridhaa hiyo ya kuwaongoza kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.
Wakizungumza na www.globalpublishers.co.tz, baadhi ya wananchi hao wamesema kuwa jarida hilo ni muhimu kwao kwani ni rahisi kusoma na kuelewa ahadi za mgombea wao, Shigongo, na namna ambavyo atazitekeleza na kuwaletea maendeleo.
“Ujue huku kwetu ni kijijini, hivyo jarida hili linaturahisishia kusoma, kuelewa na kuchambua sera bora za kiongozi tunayemtaka.
“Pia ni rahisi mimi kulisoma na kuipelekea familia yangu ama rafiki zangu nao wakasoma hata kama hawakuwepo kwenye mkutano wa kampeni basi watakuwa wameelewa kila kitu ambacho Shigongo amedhamiria kutufanyia wananchi wa Buchosa,” alisema Mpogomi John Bujingi ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Mwangika.
“Sisi akina mama wa Buchosa tunazo changamoto nyingi zinazotukabili, kwenye kilimo, vikundi, biashara, na mengine mengi. Katika jarida hili tumeona kuna mambo mengi ambayo Shigongo ameyaainisha kama vipaumbele vyake iwapo atachaguliwa. Kwa kweli yanatugusa sana sisi akina mama; ninawashauri wananwake wenzangu na Wana-Buchosa wenzangu wasome jarida hili, ambapo wataelewa nini ambacho mtu huyu amedhamiria kutufanyia,” alisema Mama Ng’weshemi.
Jarida hilo tayari limeshagawiwa katika baadhi ya wananchi wa vijiji vya Bulyahilu, Iligamba, Lushamba, Kanyala na Itulabusiga.
Pia ndani ya jarida hilo huzungumziwa maisha halisi ya Shigongo na namna ambavyo atahakikisha anatatua changamoto za wananchi wa jimbo hilo kupitia ushirikiano wao endapo watampa ridhaa ya kuwa msemaji wao ndani ya Bunge la Tanzania.
Kampeni za Shigongo zilizokuwa zizinduliwe Alhamisi ijayo, Septemba 24, 2020, zimesogezwa mbele mpaka Ijumaa, Septemba 25, 2020, ambapo zitafanyika katika Viwanja vya Nyakaliro kuanzia saa 3 asubuhi hadi saa 12:00 jioni na mgeni rasmi atakuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa na Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa.
NA DENIS MTIMA | GLOBAL PUBLISHERS