The House of Favourite Newspapers

Wasafirishaji wa Mirungi Waja na Mbinu Kujifanya Wanafunzi

WAFANYABIASHARA na Wasafirishaji wa Dawa za kulevya aina ya Mirungi wamekuja na mbinu nyingine mpya ya kujigeuza wanafunzi na kisha kuficha Mirungi katika mabegi madogo yanayotumiwa na wanafunzi kuhifadhi Daftari kwa lengo la kukwepa mkono wa askari Polisi.

 

Mbinu nyingine ambazo jeshi la Polisi mkoa wa Kilimanjaro imezigundua hivi karibuni ni pamoja na kutumia magari ya Kifahari yakiwemo Toyota Land Cruser ,Toyota Alphasad,Toyota Vanguard huku mbinu nyingine zikiwa ni kufanyia mabadiliko gari aina ya Toyota Noah ili kurahisisha ubebaji wa Mirungi kwa kificho.

 

Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro,Kamishna Msaidizi wa Polisi ,Hamis Issah alisema wasafirishaji wa Dawa za kulevya aina ya Mirungi wameendelea kubuni mbinu kila kukicha baada ya zile za awali kushtukiwa na Polisi huku akitoa onyo kwa wamiliki wa Magari ya abiria kujiingiza katika mtego wa kusafirisha dawa hizo.

 

“Hapa kuna mizigo ambayo imekamatwa na askari wetu wakiwa barabarani ,hii ni mbinu mpya ya usafirishaji ,haya mabegi unayoyaoona yote ni mabegi yanayoonesha mbebaji amebeba Madaftari anaenda shuleni ,lakini haya sio madaftari ni Mirungi ,ni mizigo iliyokamatwa kwenye mabasi tofauti tofauti”alisema Kamanda Issah.

 

Alisema katika tukio hilo watuhumiwa tisa wakiwemo wanawake wawili wamekamatwa wakiwa na jumla ya kilogramu 64 baada ya sakari Polisi kupekuwa magari matatu ya Abiria yaliyokuwa yakitokea yakiendelea na safari kutokea Moshi yakielekea Arusha.

 

“Naona mbinu zinaendelea kubadilika ndani ya wiki mbili ,mbinu tatu tofauti,kwanza ya kujaza kwenye magari,pili ya kutoboa magari kabisa,tatu kama mwanafunzi nyingine kama mtu anaenda hospitali amejifunga maplasta sasa hizi mbinu zitafika mpaka lini na sisi tunashukuru askari wangu wanafanya kazi vizuri”alisema Kamanda huyo wa Polisi Kilimanjaro.

 

Kamanda Issah amewataja wanaoshikiliwa hadi sasa kuwa ni pamoja na Ibrahim Masuli, Godfrey Richard, Chrispin Baltazar, Fanuel Hamad,na Jackline Mushi huku wengine wakiwa ni Lucy Petro ,Nuru Haruna,Silvesta Fabian naMinyari Miandei.

 

Alisema kwa sasa askari polisi wameamua kupekuwa magari yote yakiwemo ya abiria huku akiwataka abiria kutoa ushirikiano kwa jeshi l a Polisi pindi wanapoona mizigo yenye mashaka ili kuwaondolea adha ya kuchelewa kufika safari zao kutokana na usumbufu watakao pata barabarani.

 

“Tunawasihi abiria maana kuna abiria wengine wakiona askari wanapekua gari wanakasirika, msikasirike hii ndio kazi ya kupekuwa ,vinginevyo muwe mnatuambia ndani ya gari amepanda mtu wa ajabu na amebeba madawa ya kulevya aina ya mirungi hapo ndio itakuwa ni nanafuu na tutafanya kazi kwa muda mfupi li muendelee na safari,“ alisema Issah.

 

Kamanda Issah aliwataka wamiliki wa mabasi ya abiria kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi ili kuhakikisha biashara hiy inakoma kwa kukataa kubeba abiria wenye mizigo ambayo wanatilia shaka na kwamba kwa kuendelea kuwabeba itapelekea kuwaingiza katika matatizo na vyombo vyao.

 

 

“Sasa hivi sio imekuwa ni wanafunzi ambao madaftari yao ni mirungi iliyobebwa nyuma ,kwa hali kama hiyo tunawasihi wale wote wasafirishaji wa abiria kutokea Moshi kwenda Arusha wawe makini utawachelewesha abiria wako,upekuzi utaendelea na ninaelekeza askari waendelee usiku iwe mchana”alisema Issah.

 

“Kuna watu wakiona gari inapekuliwa wanatubeza ,sasa hivi tukikuona wewe unatubeza askari watakukamat,a wanawabeza askari wanaofanya kazi yao halafu tutakuhoji unatubeza kwa sababu gani,kwa hali kama hiyo tunaagiza askari waendelee kukamata mirungi na wasiiache”aliongeza Kamanda Issah.

 

Kukamatwa kwa Dawa hizo zinafanya idadi kamili ya Dawa za kulevya aina ya Mirungi zilizokamatwa katika kipindi cha wiki mbili kufikia kilogramu 564 pamoja na vyombo vya usafiri yakiwemo magari matatu na pikipiki moja.

Comments are closed.