The House of Favourite Newspapers

WASANII 5 WALIOTUMIA DAWA ZA KULEVYA

DAWA za kulevya zimekuwa changamoto kubwa katika nchi mbalimbali duniani kwani vijana wengi wamepatwa na umauti kutokana na kuathiriwa na matumizi ya dawa hizo.

 

Licha ya Serikali kuwa na nia ya dhati ya kupambana na janga hili, lakini mara kwa mara taifa limekuwa likipoteza vijana wengi ambao ni nguvu kazi kutokana na matumizi ya dawa za kulevya.

Tumeshuhudia vijana ambao tayari walishaanza kupata mafanikio, lakini ndoto zao zimekuwa zikiishia pabaya hivyo kujikuta wakigeuka kuwa na maisha ya kuwa ‘mateja’ na ombaomba barabarani.

 

Wapo ambao walikuwa wakiishi katika maisha mazuri, lakini kutokana na kujiingiza kwenye utumiaji wa dawa za kulevya wameishia kuwa tegemezi na kuomba shilingi 100 au 200 babarani. Wenyewe wanasema kupinga mzinga!

 

Lakini pia, wasanii wamekuwa wahanga wakubwa wa matumizi ya dawa hizi. Tumeshuhudia baadhi afya zao zikidhoofu na wengine kupoteza maisha. Ijumaa limekuandalia makala maalum ya wasanii ambao walitumia dawa za kulevya, lakini kwa sasa wapo poa.

TID

Nyumbani kwao wanamuita Khalid Salum Mohamed, lakini wasanii na mashabiki wake wanamtambua kama Top In Dar ‘TID’ au Mnyama.

 

Kwa muda mrefu TID alikuwa akihusishwa na matumizi ya dawa za kulevya na hata kupotea kwake ghafla kwenye muziki ilidaiwa ni kulowea katika matumizi hayo. Februari, mwaka jana katika operesheni maalum iliyoandaliwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar, Paul Makonda juu ya mastaa wanaotuhumiwa kutumia dawa hizo, alikuwa miongoni mwao na alifikia hadi hatua ya kuwekwa ‘selo’ kwa muda.

 

Siku chache mbele, katika mkutano wa kumkaribisha Kamishna Mteule wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za kulevya, Rogers William Sianga uliofanyika jijini Dar, TID alijitokeza na kuwaomba Watanzania wote wamsamahe kwa kosa alilolifanya la kutumia dawa hizo.“Nakiri nilikuwa natumia dawa za kulevya ila nimeuona mkono wa sheria umeweza kunifungua na kweli sasa hivi nipo tayari kuiunga mkono hii kampeni ili kuwaumbua watumiaji na wauzaji ili nchi iwe salama,” alisema TID.

Q Chillah

Abubakar Shaaban Katwila ‘Q Chillah’ au Q Chief naye ni miongoni mwa mastaa walioingia katika matumizi ya dawa za kulevya na kufanikiwa kujinasua.

 

Q Chillah ambaye yupo kwenye gemu la muziki wa Bongo Fleva kwa zaidi ya miaka 15, anasema sababu kubwa iliyomfanya kuingia katika matumizi hayo ni marafiki wabaya aliokutana nao ambao hawakutaka afanikiwe kipindi hicho akitamba kwenye muziki.

 

Katika moja ya mahojiano yake, Q Chillah anasema jinsi alivyoweza kujinasua; “Nilifikiri sana kabla ya kuanza kuchukua uamuzi sahihi. Ni kwamba nilikuwa nikiwatazama watoto wangu machoni naona maumivu, I saw tears (niliona machozi) wengine hawakuweza ku-handle ile situation nikajikuta nalia nao, tunalia pamoja.

 

“Lakini ikanifikia kipindi sasa nawakimbia kwa maana wakiniona wanazidi kulia, nikajiuliza nitaendelea kuwaumiza hawa malaika mpaka lini? Niliwaleta duniani na wao wawe na faraja na kesho,” anasema Q Chillah na kuongeza;

 

“Bahati iliyoje, nilikaa nao chini na kuanza kuonesha mabadiliko mwenyewe. Changes starts with you (mabadiliko yanaanza na wewe). Kwa sababu wewe unapobadilika, mtu wa jirani ataona mabadiliko yako. Lakini ukichukua muda mrefu kumuonesha jirani mabadiliko yako of course hataamini kwa sababu ukizungumzia unga naamini it’s very hard mtu kutoka. Ndiyo maana wasanii wen-zangu wanatoka, wanarudi.”

Ray C

Ni staa wa kike wa Bongo Fleva asiyesa-haulika kwenye matumizi ya dawa za kulevya. Ray C au Rehema Chal-amila mafanikio  yake yalianza akiwa na umri wa miaka 17 tu pale alipoibukia katika Radio East Africa 1999 na 2000 akajiunga na Clouds FM akiwa kama mtangazaji ambapo 2002 aligeukia kwenye muziki na kupata mafanikio makubwa.

 

Mafanikio hayo ni pamoja na kujenga nyumba nzuri na kubwa akiwa na umri wa miaka 19, baadaye kununua magari na kufungua maduka makubwa jijini Dar na hatimaye kuwa msaada mkubwa kwa familia yao. Katika mahojiano tofautitofauti na Magazeti ya Global Publishers, Ray C anasema kilicho-muingiza kwenye matumizi hayo ni marafiki wabaya na uhusiano mbaya wa kimapenzi.

 

“Ilifika kipindi, uwezo wangu wa kufanya muziki ulitoweka, nilianza kuuza vitu vyangu kimoja baada ya kingine nikianza na vidogovidogo, mwisho nikauza magari yangu, nyumba nayo ikaenda, maduka nayo nikayafilisi, nikafunga, nikaanza kuwa mtu wa kujificha huku nikiendelea kudhoofika.

 

“Nililazimika kutembea nimevaa kininja. Mungu wangu! Nilikuwa nimenasa kwenye mdomo wa mamba, dawa za kulevya zilikuwa zinanimaliza! Nilipokuja kushtuka nilikuwa tayari nimenasa, maisha yangu yakawa si starehe tena, bali mateso na aibu,” anasema Ray C na kumalizia;

 

“Nakumbuka nilivyofukuzwa kama mbwa kwa muuza dawa za kulevya kwa sababu nilikuwa sina hela, naumia sana ninapokumbuka siku nilizokuwa nalala kwenye boksi, siwezi kurudi nyumbani nikiwa arosto. Kwa sababu ya kukosa dawa kwa kukosa hela nikalazimika kulala kwenye boksi kusubiri labda itatokea kampani ininunulie dawa nipone. Yalikuwa ni mateso ya ajabu ambayo hayana mfano.”

 

Hata hivyo, Ray C alikuja kusaidiwa na Rais Mstaafu Jakaya Kikwete na kupatiwa matibabu ambayo yalizaa matunda kwa kurudi katika hali yake ambapo kwa sasa anamiliki kituo maalum cha kutoa elimu kwa walioathirika kiitwacho Ray C Foundation.

YOUNG DEE

Kama ilivyo kwa mastaa wengine, David Genzi a.k.a Young Dee naye ni miongoni mwa mastaa waliopitia katika matumizi haya na baadaye kufanikiwa kujinasua.

 

Tetesi zilianza kuvuma kuwa Young Dee amepotea kimuziki na kwamba amelowea kwenye matumizi hayo na baada ya kupita kipindi alijitokeza na kukiri kutumia.

 

“Sina mtu ambaye ninaweza kumla-umu, lakini mazingira ambayo nimepitia ndiyo ambayo yamef-anya hivyo, kuna wakati ambao nimeishi sana na watu mtaani, kwa hiyo kidogo-kidogo ikan-ifanya niweze kushaw-ishika na kuingia.

 

“Napenda kuwashauri vijana wenzangu kuwaangalia sana watu ambao wanatembea nao, ukitembea na wezi wawili na wewe utakuwa mwizi watatu, kwa hiyo tayari nimeshajitenga na watu ambao wanaweza kunishawishi na kurudi kule,” anasema Young Dee.

MSAFIRI DIOUF

Rapa huyu mkongwe wa Bendi ya The African Stars ‘Twanga Pepeta’, Msafiri Diouf naye amewahi kukiri kuwa miongoni mwa waathirika wa dawa za kulevya tangu mwaka 1996. Kama ilivyo kwa Young Dee na Q Chillah, Diouf naye alijiingiza huko kutokana na marafiki. “Nilianza kubwia unga tangu mwaka 1996, sikujua kama unga una madhara, awali nilikuwa navuta bangi, lakini kuna jamaa mmoja sasa hivi ni marehemu ndiye alinifundisha kubwia unga.

 

“Kuanzia hapo ndiyo nikafungua ukurasa mpya wa kutumia dawa za kulevya, nikafikia kipindi nikaacha kuchanganya na bangi, nikawa nabwia na kunusa, wakati ule kete moja ilikuwa ikiuzwa shilingi 250 sasa hivi inauzwa 2,000,” anasema Diouf.

 

“Nina watoto wawili, Najma a.k.a Vannesa na Taslim a.k.a Paris sasa roho iliniuma sana siku moja watoto wenzao walikuwa wanawaambia baba yenu ni teja. Nilijisikia vibaya kuona watoto wangu watazidi kusakamwa kwa kuambiwa kuwa baba yao (mimi) ni teja.

Comments are closed.