The House of Favourite Newspapers

WASANII WALIOVUMA, WAKASANDA

Image result for RAHA P
Fredinah Peyton, ‘ Rah P’

UNAWAK-UMBUKA jamaa wawili waliokuwa wakiunda Kundi la Uswahilini Matola kutoka jijini Mbeya? Unaikumbuka ngoma yao ya Kosa la Marehemu? Unayakumbuka makundi kama University Corner (UVC) lililobamba na ngoma kibao kama vile Tisheti na Jinsi na Vumilia, Kundi la Manzese Crew lililobamba na Ngoma ya Kula Kona au wadada Unique Sisters waliotikisa na Kwa Sababu Gani na Nakupenda? Hiyo ndiyo Bongo Fleva iliyotikisa mwishoni mwa miaka ya 1990 na mwanzoni mwa miaka ya 2000.

Wengi waliibuka na ngoma moja au mbili kisha wakasanda hadi leo hawajulikani walipo. Showbiz limekuandalia makala maalum kwa ajili ya wakali hawa walioibuka na ngoma moja au mbili kisha wakasanda.

Rah P

Ngoma yake ya Hayakuhusu ni miongoni mwa ngoma zinazoishi hadi sasa kuanzia miaka ya 2000 na kumfanya kuwa miongoni mwa marapa wa kike kuwahi kutokea katika Bongo Fleva. Rah P ambaye jina lake halisi ni Fredinah Peyton, baada ya kuibuka na ngoma hiyo moja tu ikatikisa vilivyo, alisanda ghafla na inaelezwa ‘alizamia’ huko Houston, Texas nchini Marekani anapoishi hadi sasa.Image result for msanii Pasha

Pasha

Ngoma ya Ni Soo ndiyo iliyomtambulisha kwenye ramani ya muziki mwishoni mwa mwaka 2007 na baadaye akaachia Thamani ya Penzi, Umeniweza kisha Hidaya. Licha ya kuanza kujijengea jina na kuonekana ni msanii pekee anayewakilisha Mtwara, Pasha alisanda ghafla. Amekuwa akihangaika kutoka tena, lakini bado haijamfanya kuwa Pasha yule wa zamani.Related image

Zay B

Kama ilivyokuwa kwa Rah P, Zay B naye alikuwa moto wa kuotea mbali kwenye Bongo Fleva mwanzoni mwa mwaka 2000. Ngoma yake na Niko Gado aliyomshirikisha Juma Nature ndiyo iliyomuweka kwenye ramani ya wakali wa Hip Hop wa kike Bongo. Baada ya kutoa ngoma kadhaa mbele kama vile Naona Noma na My Boyfriend ambazo hazikuvuma kivile, alisanda. Kwa sasa yupo na ameweka harakati za muziki pembeni.

B Boy

Ngoma ya Sina Demu akimshirikisha Stopper ndiyo iliyomsimamisha kwenye muziki na kupata shoo kibao za ufukweni enzi hizo mwanzoni mwa miaka ya 2000. Kama ilivyo kwa wakali wengine waliosanda na ngoma moja, B Boy naye alisanda baada ya ngoma hiyo tu.Image result for kali p

Kali P

Jamaa alikuwa komediani f’lan hivi kwenye muziki kwani licha ya kutoa ngoma kali pia kwenye video zake alikuwa akiburudisha kwa vituko. Ngoma yake ya Imekaa Vibaya ndiyo iliyomfanya kujulikana na kupendwa na watu wengi kwa staili yake ya kurap. Baada ya ngoma hiyo, aliibuka tena na Ngoma ya Tumbo Joto na zote akiwa amemsh-irikisha mkali wa vituko, Erick lakini mwisho wa siku alisanda na haijaju-likana hadi sasa yupo wapi.

Da Jo

Mkali huyu wa kike naye alileta ushindani kwa kukaa katikati ya rapa Zay B na Sister P ambao kipindi hicho walikuwa na bifu la kimuziki. Ngoma ya Si Ulileta Nyodo ndiyo ilimuweka kwenye chati na kuchochea ushindani kwenye muziki wa Hip Hop kwa upande wa wanawake.

Mac D

Jamaa alikuwa na sauti f’an hivi ya besi mkwaruzo na kati ya ngoma zilizomtoa miaka hiyo ya mwanzoni mwa 2000 ni Baishoo akiwa na Unique Sisters pamoja na Sugar Mumy akiwa na Dully Sykes. Baada ya kupata shoo za hapa na pale kupitia ngoma hizo, Mac D naye alisanda kwenye muziki na hajasikika hadi leo.

Fresh P

Unakumbuka Wimbo wa Tina? Fresh P alitamba sana na wimbo huo lakini baada ya muda kama ilivyo kwa mastaa wengine alisanda na kupotea kabisa kwenye ramani ya muziki hadi sasa.

Fred Saganda

Wimbo wake mmoja tu uliotoka mwanzoni mwa mwaka 2000 ulichafua hali ya hewa kwenye muziki wa Bongo Fleva. Kwanza jamaa alikuwa na staili yake ya kuimba ambapo alikuwa akiimba kwa kutumia lafudhi ya Kichaga. Alitoa wimbo mmoja tu ulioitwa Ni Jinsi Gani Tutawini Maishani na kikubwa kilicho-wavutia watu ni jinsi alivyokuwa akimuelezea Rafaeli kwenye huo wimbo.Image result for danny msimamo

Danny Msimamo

Wakati anatoka kimuziki wengi walikuwa wakimchanganya kuwa ameongeza nguvu kwenye Kundi la Wagosi wa Kaya kutoka na ukaribu aliokuwa nao. Danny Msimamo alijua kuuteka muziki na ngoma zilizompa chati ni Siku Nzuri na Nahisi. Baadaye alishirikishwa na Wagosi wa Kaya katika Ngoma ya Nyeti kisha akasanda hadi sasa.

Voice Wonder

Ni miongoni mwa wakali wa muziki waliokuwa wakiiwakilisha Dodoma sambamba na Bushoke, Ngwair, Noorah na Mez B. Voice Wonder ambaye alikuwa na sauti ya maajabu kweli, alitamba na ngoma moja ya Nimpende Nani na baadaye alitoa Ngoma ya Fatuma haikufanya poa, akasanda kwenye gemu.Related image

Dataz

Kama ilivyokuwa kwa Rah P, Da Jo na Zay B, Dataz alikuwa miongoni mwa marapa bora wa kike kuwahi kutokea Bongo miaka ya mwanzoni mwa 2000. Ngoma ya Mume wa Mtu akimshirikisha Joan ndiyo iliyomuweka kwenye chati na baadaye akaachia Wajua akimshirikisha kaka yake, Squeezer. Dataz naye alianza kusanda mapema baada ya kuingia kwenye masomo katika Chuo cha Biashara cha CBE jijini Dar.Image result for msanii besta

Besta

Kwa sasa ni mke halali wa mkongwe wa Bongo Fleva, Marlaw. Besta naye alisumbua kwenye muziki kwa upande wa wasanii wa kike na kuleta ushindani ndani na nchi za jirani. Ngoma zilizomtoa ni Baby Boy na Kati Yetu ambapo alisifika sana kwa mauno stejini na kwenye video zake. Alianza kusanda mapema, baadaye akaingia kwenye ndoa ndiyo akapotea kabisa hadi sasa.Related image

Nakaaya

Ni dada wa Miss Tanzania 2005, Nancy Sumari ambaye alitikisa kwenye Bongo Fleva na Ngoma ya Mr Politician. Nakaaya ambaye alikuwa akiwakilisha Arusha kwenye gemu, alikuwa miongoni mwa marapa wa kike wenye kujiamini hasa baada ya kuachia ngoma hiyo ambayo ilikuwa ikiegemea kwenye siasa.

Kama ilivyo kwa wengine naye alisanda na muziki ameweka pembeni hadi sasa. Wengine waliovuma wakasanda ni pamoja na Kigwema, K Basil,. Mr. Paul, Abby Skillz na wengine wengi.

Comments are closed.