WATU watano akiwemo Ofisa wa Benki ya NBC wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na kesi ya mauaji ya mwanaharakati wa ujangili, Wayne Lotter (52).
Akiwasomea mashtaka yao Wakili wa Serikali Mwandamizi, Yamiko Mlekano, amemueleza Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri, kuwa washtakiwa wanakabiliwa na makosa mawili.
Alidai kuwa washtakiwa ni Nduimana Jonas (40) ambaye ni raia wa Burundi, Godfrey Peter (42) mfanyabiashara, Innocent Pius (23) mfanyabiashara, Chambie Juma (32) mfanyabiashara na Robert Harride (31) Ofisa wa Benki ya NBC.
Washtakiwa hao wanadaiwa kutenda kosa la kula njama ya kufanya mauaji ya mtu huyo katika tarehe tofauti kati ya Julai Mosi na Agosti 16 mwaka jana.
Katika kosa la pili washtakiwa hao wanadaiwa kuwa katika makutano ya barabara za Chole na Haile Selasie, wilayani Kinondoni, Dar es Salaam, Agosti 16 mwaka jana walimuua mtu huyo ambaye ni Mkurugenzi na Mwanzilishi-Mwenza wa shirika la PALMS Foundation.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo hawakuruhusiwa kujibu chochote kwa sababu mahakama hiyo haina uwezo wa kusikiliza kesi hiyo.
Wakili Mlekano ameieleza mahakama kwamba upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika na Hakimu Mashauri ameahirisha kesi hiyo hadi Machi 6, mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.
Washtakiwa hao wataunganishwa na mfanyabiashara Rahma Almas ‘Baby'( 37 ), Mohammed Maganga (61) ambaye ni mchimba makaburi na Khalid Almas (33) wote wanaotuhumiwa katika kesi hiyo.
Comments are closed.