The House of Favourite Newspapers

Watanzania Waombwa Kujitolea Viungo vya Maiti Kuokoa Wagonjwa

JE,  umewahi kusikia kwamba baadhi ya viungo vya maiti vinaweza kuwa msaada katika matibabu ya wagonjwa wengine walio hai?

 

Kampeni mpya imeanzishwa nchini Tanzania kuhamasisha na kutoa wito kwa wananchi kuruhusu baadhi ya viungo vya ndugu zao waliofariki kuchukuliwa ili visaidie wengine walio na uhitaji wa viungo hivyo.

 

Mganga mfawidhi wa hospitali ya Mawenzi mkoani Kilimanjaro, kaskazini mwa Tanzania, Dr. Japhet Joseph,  ameliambia shirika la utanganzaji la Uingereza (BBC) kwamba jitihada zimeidhinishwa kujaribu kuwaeleimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kujitolea kuridhia kutumiwa viungo hivyo kuwasaidia wagonjwa nchini.

 

Anafafanua kuwa kuna madaktari waliobobea katika fani mbalimbali ambao wanaweza kufanya upandikizaji wa viungo vinvayoweza kuokoa maisha. Lakini tatizo linakuja wakati viungo vyenyewe kama figo, au ini au kioo cha jicho havipatikani.

 

Upandikizaji maalum wa ngozi una uwezo wa kukabiliana na saratani.   Ni kutokana na uhaba huu ndiyo kampeni imeidhinishwa kuelimisha wananchi kusudi angalau waweze kusaidia kuibadili hali na kuwasaidia wengine.

 

Dr Joseph anafananisha mchakato huo na utoaji damu ambao kampeni na uhamasishaji mkubwa umefanyika na kuwafanya watu kuchangia damu ‘kwa ajili ya kuweza kuwasaidia ndugu ambao watakuwa na matatizo’.

 

Kwa namna hiyo anaeleza kuwa wananchi watapokuwa wamepata elimu hiyo, ina maana kwamba, kama ilivyo kwa mataifa  ya Ulaya, mtu atatakiwa kusaini fomu ya kuridhia na kusema “iwapo mtu anafariki kiungo changu kitumike kumsaidia mwingine.”

Daktari anasema kuna muda ambao viungo bado viko hai baada ya mtu roho kutoka na vinaweza kutolewa na kuhifadhiwa.

 

“Ni katika muda huo ambapo vikiwahi kutolewa vinaweza kusaidia watu wengine walio hai katika upasuaji wa upandikizaji wa viungo kama inavyofanyika katika mataifa ya Ulaya na hata India. Kwa sasa ni kwamba hakuna malipo yanayotolewa kwa utoaji huo wa viungo. Anaongeza kuwa huo ni kama uchangiaji damu ambao hufanyika kwa uhisani tu wa mtu binafsi.”

 

Anasema ni watu wachache mno katika bara la Afrika walio na uelewa wa kuridhia namna hiyo na kujitolea viungo kama inavyokuwa kwa utoaji damu.

Comments are closed.