The House of Favourite Newspapers

Wateja wa Vodacom M-Pesa Wavuna Faida ya Tzs 3.9 Bilioni

0
Mkurugenzi wa M-Pesa Epimack Mbeteni akizungumza

KAMPUNI ya simu za mkononi inayoongoza kiteknolojia na kidijitali nchini, Vodacom Tanzania PLC leo imetangaza gawio la jumla ya TZS 3,928,312,789 kwa wateja wa M-Pesa ambao wametumia huduma hiyo kwa mwaka uliopita.

Malipo ya gawio hilo inahusu kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka wa fedha wa kampuni. Akiongea juu ya hili, Mkurugenzi wa M-Pesa Epimack Mbeteni alisema kuwa faida hii imekuwa ikilipwa kwa wateja, mawakala na washirika wa biashara wa M-Pesa ambao wanapokea malipo kutokana huduma/matumizi waliyofanya kupitia simu zao za mkononi. Huduma yetu ya pesa kupitia simu za mkononi, M-Pesa, inaendelea kuleta mafanikio ya kushangaza, ikiongeza thamani kubwa ya fedha kwa Watanzania.

“Tumeona ukuaji mkubwa kwenye jukwaa la M-Pesa na wateja zaidi, mawakala, wafanyabiashara na taasisi zinazofanya biashara hadi kufikia karibu TZS bilioni 100 kila siku. Tunayo furaha kushiriki katika utowaji wa gawio la Shilingi Bilioni 3.9 (sawa na Dola za Kimarekani milioni 1.6) kwa wateja wetu zaidi ya milioni 11 kote nchini, ” alisema.

Vodacom Tanzania PLC ina zaidi ya wateja milioni 11 wanaotumia huduma ya M-Pesa ikimiliki soko kwa asilimia 40, kulingana na takwimu za hivi karibuni kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA). Hadi sasa kampuni hiyo imelipa jumla ya shilingi 143.5 bilioni (zaidi ya Dola za Kimarekani milioni 62) ikiwa ni faida iliyolipwa tangu Julai 2015 wakati Benki ya Tanzania ilipotunga kanuni hiyo.

Mbeteni ameongeza kuwa sehemu ya faida kwa kila mteja imehesabiwa kulingana na kanuni za Benki Kuu ya Tanzania na itategemea, pamoja na mambo mengine, kiwango cha shughuli ambazo wateja wa M-Pesa wamefanya kwa kipindi hicho.

“Tunaendelea kulipa faida hizo kwa wateja wetu wa M-Pesa. Wateja wanaweza kutuma neno AMOUNT kwenda 15300 kwa SMS ili kujua ni kiasi gani cha riba watakachopokea. Baada ya kupokea kiasi kilichotolewa, wateja wa M-Pesa wanaweza kutumia faida hiyo kwa kununua muda wa maongezi au manunuzi ya vifurushi au hata kulipia bili au kununua bidhaa aliongeza Mbeteni.

Mnamo mwaka 2018 Vodacom M-Pesa ilipewa Hati ya Ithibati kutoka taasisi ya kimataifa inayoangalia matumizi ya Pesa kwa Simu za mkononi (GSMA) baada ya kupitishwa kwa asilimia 100 ya viwango vya ubora katika nyanja zifuatazo: kulinda fedha za wateja, usalama wa huduma, kulinda taarifa za wateja na faragha, na kudhibiti viwango vya utapeli wa pesa, kuondoa ufadhili wa kigaidi na ulaghai. Na kwa Tanzania, M-Pesa ikiwa ni bidhaa ya kwanza kabisa kuingia kwenye soko mnamo mwaka 2008. Leo uvumbuzi huu umesaidia kuongeza ujumuishwaji wa kifedha hadi 70 asilimia, kutoka 15 asilimia mnamo mwaka 2008. Huduma ya Vodacom M-Pesa ni ya hali ya juu zaidi nchini, ikiwa ni bidhaa iliyotengenezwa ili kuongeza ujumuishwaji wa kifedha nchini, huku ikichochea shughuli za kiuchumi nchini kote. Bidhaa zingine ni pamoja na; Songesha ambayo ni huduma ya mkopo ya muda mfupi, M-Koba ambayo ni akaunti ya akiba ya kikundi, Lipa Kwa M-Pesa ikiruhusu miamala ya mteja kulipia bidhaa, M-Pawaambayo ni jukwaa la akiba na mikopo na mengine mengi.

“Tutaendelea kuongoza katika ubunifu, kuleta Watanzania wengi katika uchumi jumuishi wa kidijitali, kuongeza idadi ya wateja wanaotumia huduma ya M-Pesa kupitia simu za mkononi na kupanua huduma zetu za biashara, tukizingatia ushirikiano wa kimkakati na kudumisha aina anuwai ya huduma ambazo zitarahisisha malipo ya haraka, rahisi na salama kwa Wafanyabiashara na watu binafsi vile vile, ” alihitimisha Mbeteni.

Kuhusu Vodacom M-Pesa Tanzania

Vodacom M-Pesa ni huduma ya kifedha kwa njia ya simu inayoongoza nchini iliyoanzishwa na Vodacom Tanzania PLC mwaka 2008. Kwa sasa ni moja ya huduma chache duniani zilizopewa tuzo ya ubora ya GSMA na ina wateja zaidi ya milioni 11. Kwa kiasi kikubwa M-Pesa imechangia katika kukua kwa huduma za kifedha na shughuli za uchumi nchini. Wateja wanatuma na kuweka pesa kupitia huduma ya M-Pesa kupitia kwa mawakala zaidi ya 106,000 nchini kote. Mfumo wa M-Pesa unaunganisha mabenki, makampuni na mashirika ya Serikali katika kufanya malipo ya kidigitali. Kwa sasa, M-Pesa inaendelea kuwa kinara katika soko la huduma za kifedha nchini kupitia huduma zake za kibunifu kama vile Akiba na Mikopo, malipo ya kieletroniki, huduma za vikundi na nyingine nyingi ambazo zinakidhi mahitaji ya watanzania na kuwezesha ufikaji na utumiaji Zaidi wa huduma rasmi za kifedha.

Leave A Reply