WAUMINI KICHANGANI WAOMBOLEZA MJENZI WA MSIKITI

WAISLAM wa Kichangani, Magomeni Mapipa, Dar es Salaam, jana walimiminika katika msikitI wa Kichangani katika sala ya kumwombea marehemu Sheikha Hessa binti Muhammad Nahyan aliyejenga msikiti huo na misikiti mingine 300 barani Afrika na duniani.
Mama huyo wa heshima aliyekuwa raia wa Falme za Kiarabu alifariki juzi na kuzikwa siku hiyohiyo jijini Abu Dhabi ambapo kutokana na kifo chake hicho taifa hilo limetangaza maombolezo ya siku tatu.

Kiongozi wa msikiti wa Kichangani, Musa Yusuph, alisema baada ya kupokea taarifa za kifo chake, waumini walikusanyika na kuswali sala ya mauti iliyofanyika magharibi ili kumuombea kwani ni mama aliyejenga msikiti huo ikiwa ni pamoja na majengo yote ya shule ya chekechea na msingi ambayo yalipewa jina lake la Sheikhat Hessa Islamic Nursery School na Sheikhat Hessa Islamic Primary School.
“Mama huyo amefanikiwa kujenga misikiti mingi lakini kwa Tanzania alijenga msikiti huu wa Kichangani wenye uwezo wa kusalisha waumini elfu tano ambapo huko Zanzibar alijenga msikiti wa Jibril unaofanana kabisa na huu. Kwa kifupi ameacha sadaka nzuri kwa waumini wa Kiislamu.
“Pamoja na kujenga msikiti huu mama huyo hakuwahi kufika kuuona bali alikuwa akiwatuma wawakilishi ambao waliuona na kuupiga picha. Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi, Amen!” alisema Yusuph.


Comments are closed.