Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wiliam Lukuvi ametoa Miezi sita kwa Mkurugenzi wake kusimamia zoezi linaloendelea la usimikaji na uendeshaji wa mradi wa mfumo wa Kielekitroniki Unganishi wa Taarifa za Ardhi.
Hayo ameyasema leo Jumatatu, Novemba 22, 2017 wakati alipotembelea zoezi hilo linaloendelea katika wizara yake ambapo alisema kuwa mradi huo unadhaminiwa na Benki ya Dunia.
Amesema kuwa lengo kubwa la mradi huo ni kuimarisha usalama katika umiliki wa ardhi kwa kuboresha usalama na usahihi katika manunuzi ya ardhi na kuanzisha mfumo sahihi na imara wa taarifa za ardhi.
Ameeleza kuwa mradi huo unatekelezwa katika Kanda ya Dar es Salaam na Manispaa ya Kinondoni na utahusisha usimamizi wa ardhi, usajili, upimaji na kusaidia katika mchakato wa kuhamisha taarifa za ardhi na ramani katika mfumo wa kielekitroniki.
Aidha, Lukuvi alisema kuwa anamwomba ifikapo Juni Mosi mwakani angalau mfumo huo uwe tayari kwa kuanza kutumika.
NA DENIS MTIMA | GPL