The House of Favourite Newspapers

Waziri Mkuu Mstaafu Pinda Afurahishwa na Ilipofikia VETA

Waziri Mkuu Mstaafu Pinda akizungumza na wanahabari (hawapo pichani) baada ya kutembelea kwenye kongamano la miaka 30 ya VETA.

Dar es Salaam, 20 Machi 2025: Waziri Mkuu Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda, leo ametembelea kwenye kongamano la maadhimisho ya miaka 30 ya VETA linaloendelea kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere JNICC Jijini Dar, na kuonesha kufurahishwa na aliyojionea.

Waziri Mkuu Mstaafu Pinda alifika kwenye kongamano la maadhimisho hayo na kujionea mambo mbalimbali ya kiteknolojia ikiwemo mifumo ya umeme, uchongaji, uhandisi majengo, mifumo ya maji, ushonaji, ufundi vyuma, useremala, upishi, ushonaji kilimo, ufugaji na mengineyo.

Waziri Mkuu Mstaafu Pinda (kulia) akimuangalia kijana asiye na mikono anavyochora ramani ya jengo kwa kutumia miguu baada ya kupata ujuzi wa kusanifu majengo kutoka VETA.

Baada ya kujionea mambo mbalimbali ya kibunifu kwenye mabanda ya maonesho Pinda aliisifu VETA ilipofikia na kusema kama tukiendelea hivi na kujiboresha zaidi kiteknolojia basi tutafika mbali na itakuwa ndiyo ukumbozi wa taifa letu.

Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore (kulia) akimuelekeza jambo Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore amemshukuru Waziri Mkuu Pinda kwa kuweza kufika kwenye kongamano hilo na kujionea kinachoendelea VETA.

Waziri Mkuu Mstaafu, Pinda akipata maelekezo kutoka kwa mmoja wa wanafunzi wa VETA.

CPA Kasore amesema si kwamba, Waziri Mkuu Mstaafu Pinda ni mgeni VETA bali amefika kwenye kongamano kujionea ilipofikia maana akiwa Waziri Mkuu alihusika kusimamia maboresho makubwa yaliyoifikisha VETA hapa ilipofikia. HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS NA NEEMA ADRIAN /GPL