Waziri mkuu wa zamani wa Israel ahukumiwa kwenda jela
Ehud Olmert
Jerusalem, Israel
Mahakama Kuu ya Israel, imemhukumu aliyekuwa waziri mkuu wa nchi hiyo kuanzia mwaka 2006-2009, Ehud Olmert kifungo cha miezi 18 jela baada ya kukutwa na hatia kwenye makosa ya kula rushwa yaliyokuwa yanamkabili.
Awali, Mei, 2014, Olmert alihukumiwa kifungo cha miaka 6 jela kufuatia kukutwa na hatia katika makosa ya kupokea rushwa katika kipindi cha 1993 hadi 2003 alipokuwa Meya wa Jiji la Jerusalem. Baada ya hukumu ya awali, Olmert alikata rufaa na baada ya mahakama kupitia upya shauri lake, bado imemkuta na hatia ila amepunguziwa kifungo.
Olmert anatarajiwa kuanza kutumikia kifungo chake, Februari 15, 2016 na atakuwa ndiye kiongozi wa kwanza wa juu wa nchi hiyo kufungwa jela.
“Nilishasema kuanzia awali, sikuwahi kutoa wala kupokea rushwa. Naheshimu maamuzi ya mahakama,” alisema Olmert baada ya hukumu hiyo.
Waziri mkuu huyo wa zamani, anadaiwa kupokea rushwa wakati wa ujenzi wa mji mtakatifu wa Jerusalem na pia kutumia vibaya madaraka yake kwa kufanya biashara na rafiki yake wa karibu, Uri Messer akiwa kiongozi wa serikali.