Waziri Nape alivyohitimisha ziara Kanda ya Ziwa

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye amehitimisha ziara ya kukaguwa ujenzi wa minara ya mawasiliano kwa mikoa mitano ya Kanda ya Ziwa.
Ziara ya Nape ilianza Julai 15 mkoani Kigoma na akaelekea Mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza na Julai 19, 2024 amemalizia mkoani Shinyanga.
Minara aliyokuwa akikaguwa ni miongoni mwa minara 758 inayojengwa katika mikoa 26 ya Tanzania Bara ambayo itawanufaisha zaidi ya watanzania waishio Vijijini wapatao milioni 8.5 kupitia mradi unaosimamiwa na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF).
UCSAF ambayo ni taasisi ya Serikali chini ya Wizara ya Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari inatoa ruzuku ya fedha kwa makampuni ya mawasiliano nchini ambayo yanakwenda kujenga minara katika maeneo ya wananchi wa vijijini ili wapate huduma bora za mawasiliano.
Mikoa hiyo mitano inajengwa minara 117 katika kata 113 huku vijiji 240 vikinufaika na wanakijiji zaidi ya 1.86 milioni wanatarajiwa kunufaika na huduma ya mawasiliano kwa teknolojia 2G, 3G na 4G.
Nape leo amehitimisha kwa kukagua minara miwili mkoani Shinyanga iliyojengwa na Kampuni ya Mawasiliano ya Halotel katika Kijiji cha Busangwa wilayani Kishapu na mnara uliojengwa na Tigo katika Kijiji cha Ngokolo wilayani Ushetu ambayo yote miwili serikali imechangia ruzuku ya Sh257.46 milioni.
Akizungumza na wananchi katika vijiji mbalimbali alivyotembelea Waziri Nape amewaeleza faida za mawasiliano kwenye uchumi wa kidigitali ni nyingi ikiwemo ufanisi wa biashara, upatikanaji wa masoko mapya pia kuimarisha ajira.
Faida nyingine ni ufikiaji wa habari, kuboresha ubunifu, kuongeza pato la taifa, kuwiana kwa fursa na uendeshaji wa biashara ndogo ndogo.
“Teknolojia ya kidigitali inarahisisha shughuli za biashara, kupunguza gharama, na kuongeza ufanisi katika uzalishaji na utoaji wa huduma. Uchumi wa kidigitali unafungua fursa kwa biashara kufikia masoko ya kimataifa, hivyo kuongeza mauzo na mapato.” Alisema Nape.