Wema Ala Shavu Tatu Mzuka
UNAWEZA kusema huu ni mwaka wa neema kwa staa wa Filamu Bongo, Wema Sepetu, kwani baada ya wiki iliyopita kulamba dili la Kombe la Dunia kutoka kwa StarTimes, leo tena amelamba shavu jipya kutoka Kampuni ya The Network ambayo ni kampuni mama inayoendesha mchezo wa namba wa Tatu Mzuka nchini kwa kumtangaza kuanzisha naye ushirikiano wa kibiashara.
Akizungumza wakati wa kumlambisha shavu hilo rasmi, mkuu wa kitengo cha mawasiliano wa Tatu Mzuka Sebastian Maganga, alisema ushirikiano wao na Wema ni mpango mkakati wa Tatu Mzuka wa kufanya kazi bega kwa bega na Watanzania ili kuboresha maisha yao.
“Kusudi kubwa la Tatu Mzuka kuingia makubaliano na Wema, ina lengo la kutaka kusambaza fursa kwa watu wengi kadri iwezekanavyo ili kuboresha maisha yao ya kila siku.
“Ushirikiano huu ni kati ya ushirikiano mbalimbali ambao tumekuwa tukijihusisha nao huko nyuma, hivyo basi Watanzania watambue kuwa muda mwingi tunaangalia kipaji kipi ambacho tunaona kinaendana na bidhaa yetu na kuanzisha ushirikiano kwa kibiashara kama ilivyo leo hii kwa Wema,” alisema Maganga.
Kwa upande wake Wema amesema kuwa: “Nina hamu kubwa ya kuanza kuwashirikisha bidhaa hii mashabiki zangu wote na Watanzania kwa ujumla wao ili waweze kujitengenezea fursa nyingi za kuboresha maisha yao kupitia kwangu.
“Hivyo ningependa kuanzia sasa mashabiki zangu wote wachangamkie Tatu Mzuka kwa kucheza kwa njia ya kuingiza namba ya kampuni ambayo ni 555111 na baada ya hapo unaweka namba zako tatu za bahati kisha unaandika jina langu yaani WEMA na unaingiza kuanzia kiasi cha shilingi 500 hadi kiasi kisichozidi elfu 30,000, kisha unatuma na utakuwa umejipatia nafasi kubwa ya kushinda hadi shilingi milioni 260,” alisema Wema.
Stori: Musa Mateja | Global Publishers
Comments are closed.