The House of Favourite Newspapers

Wema Atapata Mtoto Mwakani

0

NATAMBUA uchungu alionao Wema Sepetu wa kukosa mtoto, lakini namwambia huko aliko aisikie sauti ya Mungu, mwakani atapata mtoto.”

Kauli hii ilitolewa juzi (Jumanne) na Nabii Bendera ambaye ni Mchungaji wa Kanisa la Pentecoste lililopo Kimara jijini Dar es Salaam, alipozungumza na Gazeti la Amani kwa njia ya simu.

 

Mwandishi wetu alimuuliza Nabii Bendera anaichukuliaje kauli ya Miss Tanzania 2006, Wema Sepetu aliyoitoa hivi karibuni kupitia App yake iitwayo Wema kuwa hawezi kuzaa kwa sababu ana laana.

Wema alisema laana hiyo ameipata baada ya kutoa mimba mbili za aliyekuwa msanii wa filamu nchini, Marehemu Steven Kanumba.

 

Kufuatia kauli hiyo, Nabii Bendera alisema:

“Wema hana tofauti na Hana wa nyakati za Biblia ambaye alitafuta mtoto kwa muda mrefu lakini hakupata hadi alipokutana na neno la mtumishi wa Mungu akapata mtoto.

 

“Ukisoma maandiko kwenye kitabu cha 1Samweli 1:10-20 utaona kisa cha huyo mwanamke aliyekuwa na uchungu wa kukosa mtoto, lakini baada ya kufanya maombi ya muda mrefu yaliyoambatana na kilio, Mungu alimpatia mtoto.

 

“Mungu wa Hana ndiyo huyohuyo Mungu wa Wema, anachotakiwa kufanya Wema ni kuungama kwa Mungu kosa lake na hiyo inayoitwa laana. Itafutwa na yeye anatakiwa kuisahau, akifanya hivyo bila shaka majira kama haya mwakani atapata mtoto,” alisema Nabii Bendera huku akimtaka pia kusoma neno katika Kitabu cha 2Wafalme 4:6.

 

Ambayo kwa ufupi maandiko yanasomeka hivi: “Kisha Elisha akasema: Wakati huu, mwaka ujao, utakuwa ukimkumbatia mwana.”

Hata hivyo, Nabii Bendera aliongeza kuwa pamoja na Wema kutafuta mtoto, lazima atambue kuwa mtoto hapatikani kwa njia ya maneno, bali matendo.

 

“Hana alipoomba hakubaki na maneno, alikwenda kushiriki tendo na mumewe na huko ndiko alikopata ujauzito.

“Sasa huyo Wema mimi simjui vizuri kama ameolewa au la, kama hajaolewa lazima maombi yake yaambatane na matendo matakatifu,” alisema Nabii Bendera.

 

Kuhusu njia gani anayoweza kutumia Wema na kusamehewa hiyo anayoiita laana ya Kanumba, Nabii Bendera alisema:

“Ujumbe huu ninaokupa ni unabii halisi, akiusikia aje kanisani tuombe pamoja na Mungu atasikia maombi yetu bila shaka na mwakani atakumbatia mtoto.”

 

Hivi karibuni mama mzazi wa marehemu Kanumba, Flora Mtegoa aliangua kilio baada ya kusikia Wema akikiri kuwa amewahi kutoa mimba mbili za Marehemu mwanaye.

 

“Jamani mpaka nywele zilinisisimka kabisa, natamani sana kuongea na Wema nikae naye maana uzuri ni kwamba amekiri mwenyewe kuwa alitoa mimba za mwanangu, yaani imeniumiza sana jamani,” alisema mama Kanumba alipozungumza na gazeti dada la hili Ijumaa Wikienda wiki iliyopita.

 

Mama Kanumba amemuomba Wema washirikiane pamoja katika kuomba ili hicho kinachoitwa laana ya Kanumba kiweze kuondoka na kumfanya msichana huyo kupata mtoto.

Gazeti la Amani lilimtafuta Wema kwa njia ya simu ili kujua kama yuko tayari kwenda kanisani kwa Nabii Bendera kushiriki maombi ya kuvunja laana hiyo, hakuweza kupatikana.

Stori: Mwandishi Wetu, Amani

Leave A Reply