The House of Favourite Newspapers

WEMA SEPETU AMZABA MAKOFI CHARLES BABA

Wema Isaac Sepetu

KIBANO! Ndivyo unaweza kusema kufuatia kitendo alichofanya mwanadada kipenzi wa Watanzania, Wema Isaac Sepetu cha kumzaba vibao mpenzi wake wa zamani, Charles Gabriel ‘Chaz Baba’ kisa kikiwa ni msanii wa Bongo Muvi, Husna Idd ‘Sajenti’.

Mtiti huo ulitokea usiku wa kuamkia Jumatatu iliyopita kwenye ukumbi wa burudani wa The Club Legend (zamani Nyumbani Lounge), ambapo Bendi ya The African Stars ‘Twanga Pepeta’ ilikuwa ikikamua katika moja ya shoo zake za wiki.

ILIKUWA HIVI

Baada ya Chaz Baba kuburudisha jukwaani na wanamuziki wenzake, alishuka na kwenda maliwatoni, wakati akitoka huko alikutana na Wema njiani na baada ya mazungumzo machache, wapenzi wa burudani walishuhudia mlimbwende huyo aliyewahi kutwaa Taji la Miss Tanzania 2006 akimzaba makofi kadhaa Chaz Baba.

KALALA AMTOA

Wakati tukio hilo likizua taharuki ukumbini hapo, msanii mwenzake na Chaz Baba, Kalala Hamza ‘Junior’ ambaye alikuwa karibu, alimsogelea Wema na kumtoa nje ya ukumbi kwa kusaidiana na msaidizi wa karibu wa Wema aitwaye Agrey.

RISASI LAMVAA WEMA

Wakati Wema akiondoka Risasi Mchanganyiko, ambalo lilikuwa ‘busy’ kufuatilia matukio yaliyokuwa yanaendelea ukumbini hapo lilimvaa ili kufungukia kile ambacho kilikuwa kimetokea. Lakini baada ya kuulizwa, Wema alijibu kwa maneno mawili tu ya Kingereza; “No comment.” Risasi Mchanganyiko, lilijaribu pia kumbana lakini alikataa katakata kuzungumza lolote lile zaidi ya hapo.

CHAZ BABA AFUNGUKA

Kwa upande wa Chaz Baba, baada ya kufuatwa ili kuzungumzia tukio hilo, alisema kwamba hata yeye mwenyewe alishangazwa na kitendo alichokifanya Wema kwani hakukitegemea. “Tulikuwa vizuri tu maana jioni tulikuwa naye pamoja kwenye kikao cha kamati ya Miaka Ishirini ya Twanga maana na yeye ni mjumbe, tunategemea kusherekea naye siku hiyo kwa sababu itakuwa ni siku yake ya kuzaliwa pia usiku huo.

“Hakukuwa na shida yoyote. Sasa nimeshuka jukwaani naenda maliwatoni mara nikakutana naye akaanza kuniuliza kwa nini Sajenti ananiposti kwenye mitandao ya kijamii na kwa nini tupo karibu. “Mimi nilimjibu kuna shida gani kwa sababu nina uhuru wa kuwa karibu na mtu yeyote yule na yeye hawezi kunipangia masharti kwa sababu si mpenzi wangu.

“Nilipomjibu tu hivyo nilishitukia nazabwa makofi kadhaa usoni. Kalala alikuwa karibu ikabidi amtoe. Kiukweli ni kwa sababu ni mwanamke lakini angekuwa mwanaume mwenzangu pangechimbika,” alisema Chaz Baba.

Risasi Mchanganyiko, lilimuuliza kama amerudiana na Wema lakini alikataa juu ya hilo na kuongeza kwamba kuhusu Sajenti hawezi kuacha kuwa naye karibu kwa sababu mbali na kuwa si wapenzi lakini bado atabakia kuwa mzazi mwenzake.

Risasi Mchanganyiko lilijaribu kumtafuta Sajenti ili kumsikia anazungumziaje ishu hiyo lakini simu yake haikupokelewa hadi tunakwenda mitamboni.

STORI: Boniphace Ngumije, Risasi Mchanganyiko

Comments are closed.