The House of Favourite Newspapers

Wilaya ya Chemba Yaahidi Kutatua Changamoto za Elimu

0
Mwenyekiti wa Mtandao wa Elimu (TEN/MET), Dk. John Kalage (katikati) akihutubia kwenye hafla ya kufunga Maadhimisho ya Juma la Elimu nchini yaliyofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Msingi Chemba. Kushoto ni Mgeni rasmi na Afisa Tarafa ya Goima, Bi. Rhobi Stephano pamoja na Mratibu wa Taifa wa TENMET, Bw. Ochola Wayoga (kulia) wakifuatilia.
Mgeni rasmi Afisa Tarafa ya Goima, Bi. Rhobi Stephano (kulia) akipata maelezo kwenye Banda la Mtandao wa Elimu Tanzania (TENMET) alipotembelea mabanda ya taasisi wanachama wa mtandao huo, kwenye hafla ya kufunga Maadhimisho ya Juma la Elimu nchini yaliyofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Msingi Chemba. Wa pili kulia ni Mwenyekiti wa Mtandao wa Elimu (TEN/MET), Dk. John Kalage pamoja na Mratibu wa Taifa wa TENMET, Bw. Ochola Wayoga.
Rhobi Stephano (kulia) akipata maelezo ndani ya Banda la Mtandao wa Elimu Tanzania (TENMET) alipotembelea mabanda ya taasisi wanachama wa mtandao huo.
…Bi. Rhobi Stephano (kulia) akipata maelezo ndani ya Banda la Uwezo Tanzania namna wanavyotekeleza miradi mbalimbali alipotembelea mabanda ya taasisi wanachama wa mtandao huo.
Mgeni rasmi Afisa Tarafa ya Goima, Bi. Rhobi Stephano (wa pili kushoto) akikabidhiwa fomu y kujiunga na marafiki wa elimu ndani ya Banda la Haki Elimu alipotembelea mabanda ya taasisi wanachama wa mtandao huo, kwenye kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu nchini yaliyofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Msingi Chemba. Anaye mkabidhi ni Mwenyekiti wa Mtandao wa Elimu (TEN/MET), Dk. John Kalage, ambaye pia ni Mkurugenzi wa HakiElimu.
Baadhi ya wanafunzi wa msingi na sekondari wakiangali video ya mafunzo ndani ya Banda la Uwezo Tanzania, kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu nchini yaliyofanyika wilayani Chemba.
Wanafunzi wa Shule ya Msingi Chemba wakitoa burudani kwenye kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu.

 

SERIKALI wilayani Chemba imeahidi kuzifanyia kazi changamoto za elimu ya msingi na sekondari zilizoibuliwa katika mijadala ya Maadhimisho ya Juma la Elimu lililofanyika wilayani hapo kwa kukutanisha wadau anuai wa elimu nchini.

 

 

Kauli hiyo imetolewa juzi na Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Simon Chacha  katika hotuba yake iliyosomwa na Afisa Tarafa ya Goima, Bi. Rhobi Stephano akimwakilisha katika hafla ya kufungwa kwa Maadhimisho ya Juma la Elimu nchini zilizofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Msingi Chemba mjini hapa.

 

 

Alisema Serikali inaushukuru Mtandao wa Elimu Tanzania (TENMET) na wadau wote kwa kuleshughuli za Maadhimisho ya Juma la Elimu wilayani Chemba kwani uamuzi huo ni kuipa kipaumbele wilaya hiyo ili iweze kufanya vizuri zaidi katika sekta ya elimu. Aliongeza kuwa jitihada zinazozifanywa na Serikali kuinua elimu lazima ziungwe mkono na wazazi wa eneo husika, wadau wa elimu na wananchi kwa ujumla ili ziweze kuleta mafanikio.

 

“…Serikali haiwezi kufanya mambo haya peke yake bila wazazi na wadau wa elimu kuunga mkono, na hili lipo wazi hata ukiangalia maeneo mengine ambayo nguvu za wananchi na Serikali zikiungana sekta ya elimu inafanya vizuri kuanzia miundombinu na hata ufaulu wa wanafunzi,” alisema Bi. Stephano akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Chemba.

 

Aidha alisema Serikali ya Wilaya inaahidi kuzifanyia kazi changamoto zote zilizoibuliwa katika mijadala ya elimu katika juma la maadhimisho na kuwaomba wazazi na wananchi waeneo husika kushirikiana na viongozi kutatua changamoto hizo.

 

Akizungumza awali, Mwenyekiti wa Mtandao wa Elimu (TEN/MET), Dk. John Kalage alisema  Maadhimisho ya juma la Elimu wilayani Chemba, yamepata mafanikio makubwa kutokana na mapokezi na ushirikiano mzuri wa viongozi na watendaji wa serikali, wanajamii, walimu na wanafunzi.

 

Alibainisha kuwa, muitikio huo wa jamii unadhihirika pia katika baadhi ya miradi inayotekelezwa na jamii za shule husika zikiwemo, Kushiriki ujenzi wa miundombinu ya shule yakiwemo Mabweni, Vyumba vya madarasa, nyumba za walimu, ujenzi wa Vyoo, na kusaidia jitihada za upatikanaji wa maji na hata kuchangia huduma za vyakula kwa wanafunzi wakiwa shuleni, Ingawa bado kuna changamoto katika suala la ushiriki wa wananchi kukamilisha miradi.

 

Alizitaja baadhi ya changamoto zilizoibuka katika mijadala kuwa ni upungufu wa maabara na vifaa vya maabara, upungufu wa vitabu, walimu na nyumba za walimu, upungufu wa matundu ya vyoo, uhaba wa maji safi na salama kwa wanafunzi na walimu, upungufu wa madawati, pamoja na ukosefu wa nishati ya umeme.

 

“Wanafunzi wengi bado wanatembea umbali mrefu kufika shuleni na kurejea nyumbani, ambapo baadhi yao wanatembea kilomita takribani sita mpaka kumi na tano kwa siku. Changamoto hii imejidhihirisha zaidi kwa wanafunzi wa shule za sekondari. Hali hiyo huwafanya wanafunzi kuchelewa shuleni, kuchoka na kukosa muda wa kujisomea na kusababisha utoro wa rejareja.”

 

Hata hivyo,  Dk. Kalage alisema mtandao unapendekeza uwajibikaji wa pamoja katika kuifikia elimu bora na jumuishi; hivyo ipo haja ya Serikali, jamii na Wadau  kuongeza jitihada zaidi za kujenga miundombinu ya kutosha kwa wanafunzi na walimu, ilhali jamii iendelee kuhamasishwa kuithamini elimu na kuchangia nguvu kazi na raslimali katika kuboresha elimu na kufuatilia maendeleo ya watoto wao.

 

Leave A Reply