NANI kasema Rais Dk. John Magufuli kabana kwenye suala la mkwanja? Kama wewe unaamini hivyo basi habari ikufikie kuwa, staa wa filamu Bongo, Jacqueline Wolper amempiga kigogo mmoja aliyewahi kuwa bwana wake (jina linahifadhiwa) kiasi cha shilingi milioni 100 na kufanyia mambo makubwa ikiwemo kufungua bonge la ofisi lililopo Kinondoni Mkwajuni jijini Dar, Risasi Jumamosi lina ‘pakeji’ ya kutosha.
Taarifa za awali zilizolifikia gazeti hili zilidai kuwa, mwanadada mchanga anayejua kuitafuta pesa amefungua bonge ya ofisi iliyomgharimu mamilioni ya pesa huku wengi wakihoji amezipata wapi wakati hali ya kiuchumi kwa mastaa wengi ni mbaya?
“Jamani Wolper kafanya kufuru ya aina yake, kafungua ofisi ya gharama, kama milioni 300 zimetumika na ndani yake kuna biashara kibao, yaani siyo bure lazima kutakuwa na kigogo aliyemgharamia maana kwa hali ilivyo, hana ujanja wa kufanya yote haya, fuatilieni muone wenyewe,” alisema mmoja wa watu wa karibu wa staa huyo aliyeomba hifadhi ya jina lake.
RISASI LAMFUNGIA KAZI
Baada ya kupata habari hizo, gazeti hili lilimfungia kazi staa huyo ambapo kwa kuanzia mapaparazi wetu waliitafuta ofisi hiyo na kubaini kuwa ipo Kinondoni hivyo kupiga picha kadhaa kwa nje kisha kuanza jitihada za kumtafuta.
AIBUKIWA OFISINI KWAKE
Baada ya kuipata ofisi hiyo, waandishi wetu walimpigia simu na kutaka kuonana naye ambapo bila hiyana aliwaruhusu kufika ofisini kwake kwa mahojiano.
ALIWEZAJE KUJENGA OFISI HIYO?
Akizungumza na Risasi Jumamosi ndani ya chumba ambacho ukutani kimepambwa na nyaraka mbalimbali za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Wolper alisema kuwa alipata wazo la kuwa na ofisi yake ya mambo ya mitindo na ushonaji miaka miwili iliyopita na alianza kubuni jinsi litakavyokuwa ndipo akaanza taratibu mpaka kufikia hapo.
“Unajua mimi nikiamua kufanya jambo huwa nalifanya na hulianza taratibu mwisho hufanikiwa ndiyo maana na hii nikaiweza,” alisema staa huyo kwa kujiamini.
AMPIGA KIGOGO MIL. 100
Alisema kuwa katika pesa alizotumia, kiasi cha shilingi milioni 100 alizipiga kutoka kwa kigogo mmoja ambaye alitokea kumpenda aliyempa akanunue vito vya dhahabu na simu kali lakini kwa ujanja akazipeleka kuimarisha ofisi hiyo.
“Unajua nilipompata yule bwana kipindi hicho alinikuta kwenye ‘stress’ sana, nilikuwa nimeachana na mwanaume ambaye aliniumiza hivyo alinifuta machozi.
“Nilikuwa nikiishi hotelini huku nina milioni mia moja zangu kwenye sefu nikiwa mimi na mdogo wangu, hapohapo ndiyo nilipata akili ya kuamua nifanye nini kwa ajili ya maendeleo bila kumshirikisha yeye,” alisema Wolper.
AJENGA TARATIBU
Akaongeza kuwa, alipoona amefikia pazuri alimchukua yule bwana na kwenda kumuonesha alichokuwa akifanyia pesa anazochukua kwake, ndipo mwanaume huyo akafurahi na kumuongezea kiasi kingine cha pesa.
“Nilipompeleka akaona hatua za mwanzo za ujenzi jinsi nilivyokarabati ile nyumba niliyopanga kwa ajili ya ofisi, alifurahi akaamua kuniongezea pesa nyingine,” alisema Wolper.
BWANA ASHTUKIA ANAPIGWA, AINGIA MITINI
Staa huyo alizidi kuweka wazi kuwa, bwana huyo aliingia mitini baada ya kugund u a kuwa a n apigwa pesa hasa baada ya picha ya kimahaba inayomuonesha Wolper na mwanaume mwingine kuvuja.
“Huwezi kuamini mpaka leo natamani kumuona yule bwana ambaye alinipa zile pesa, alipotea kwenye mazingira ya kutatanisha. Aliniita na kuniambia kuwa nitamtafuta sitampata.
“Hamuwezi kuamini nilipiga ile simu mpaka kesho sijawahi kumpata bwana yule,” alisema Wolper.
ATOA FUNZO KWA MASTAA WENZAKE
Akitoa fundisho kwa mastaa wenzake, Wolper aliwashauri kutumia vizuri wanaume wanaokutana nao katika safari ya kimapenzi kwani yeye alikuwa mjanja, akamtumia vizuri kigogo huyo na sasa ana mafanikio makubwa.
“Unajua siyo kila pesa unayopewa na mpenzi unatumia kwenye anasa, kama akikupa ununue gari unaangalia la bei nafuu kisha unawekeza kwenye vitu vingine vya maana, hivihivi si rahisi kupata maendeleo.
“Kwa sasa nashona nguo za aina zote ikiwemo za maharusi, matirio za nguo zangu zinatoka nje ambapo ninao mawakala washkaji zangu nchini India, hao huwa wananitumia na Burundi vitenge napata original kabisa,” alisema Wolper.
ANA MALENGO MAKUBWA
Huku akionekana kweli kabadilika, yaani siyo yule Wolper chapombe tena, staa huyo alisema kuwa kwa sasa ana malengo makubwa ikiwa ni pamoja na kufungua kampuni itakayokuwa inajishughulisha na usafambazaji wa vyakula vya aina mbalimbali zikiwezo nafaka.
“Watu hawawezi kuamini, Wolper huyu ni mwingine kabisa si yule mnayemjua. Sasa hivi niko bize nafanya kazi mpaka usiku na wakati mwingine nikiwa na kazi nyingi hujikuta naweka kigodoro na kulala ofisini ilimradi tu nimalize kazi za watu kwani kwenye ufundi kuna changamoto nyingi sana,” alisema Wolper huku akiongeza kuwa, hivi sasa mafundi nguo watammisi kwani awali alikuwa akitumia pesa kushonesha lakini sasa anavaa nguo anazoshona mwenyewe.
WEMA, KAJALA, UWOYA WANASUBIRI
Kwa hatua aliyofikia mwanadada huyo, ni wazi kwamba mastaa kama vile Wema Sepetu, Kajala Masanja na Irene Uwoya ambao kwa nyakati tofauti waliwahi kufungua ofisi zao, watakuwa na kazi kubwa ya kufikia mafanikio aliyonayo Wolper kwa sasa.
STORI: HAMIDA HASSAN NA GLADNESS MALLYA, RISASI JUMAMOSI