Wolper; Mama wa Dogodogo!
MIAKA 15 iliyopita, binti wa Kichaga, aliyekuwa na umri wa miaka 18 tu, alifunga safari kutoka nyumbani kwao, Machame kule Moshi mkoani Kilimanjaro na kwenda jijini Arusha kutafuta maisha. Ilikuwa ni baada ya kumaliza elimu ya msingi na sekondari.
Huyu si mwingine, bali ni Jacqueline Wolper Massawe ‘Wolperstylish’. Akiwa Arusha, Wolper alisoma masomo ya biashara kabla ya kutinga jijini Dar katika harakati za kusaka maisha.
Alipofika Dar, hapo ndipo alipoanza kuparangana na shughuli za saluni kisha kuzama kwenye tasnia kubwa ya filamu za Kibongo.
Shukrani ziende kwa mwigizaji Lucy Komba ambaye ndiye aliyemuingiza kwenye ulimwengu wa filamu za Kibongo.
Baadhi ya filamu ambazo Wolper amefanya poa ni pamoja na Tom Boy–Jike Dume, Crazy Desire, Mahaba Niue, I am Not Your Brother, Chaguo Langu, Dereva Taxi, Shoga Yangu, Family Tears na nyingine kibao kabla ya kuzipa kisogo na kuanzisha kampuni ya mitindo ya nguo ya Wolperstylish.
Lakini yote kwa yote unapokuwa staa, ina maana wewe ni kioo cha jamii na jamii inakuangalia kwa kila unachokifanya. Hivyo, ni jambo la kuwa makini kwa kila unachokifanya.
Wapo mastaa wengi wa kike Bongo ambao wamewahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi na wanaume ambao ni wadogo kwao kiumri (ben’teni), lakini walipogundua, waliacha na kama hawakuacha, basi wamekuwa wakificha uhusiano wao.
Kwenye orodha ya mastaa hao wa kike, anayeonekana kuwa kinara kwa kutoka kimapenzi na ‘wadogo zake’ ni Wolper ambaye amezaliwa Desemba 6, 1987. Kwa sasa ana umri wa miaka 33.
Wolper ni mrembo ambaye ana vigezo vya kumvutia mwanaume yeyote rijali na kutamani kuwa naye, lakini kwenye orodha ya wapenzi aliowahi kutoka nao, asilimia kubwa inaonekana kiumri ni wadogo zake, hivyo mitandao ya kijamii kumpachika jina la Mamaa wa Dogodogo!
Japokuwa mapenzi hayachagui umri, lakini ni jambo la kuangalia wewe unayefanya ni nani, unatazamwa na watu gani kwenye familia inayokuzunguka? Ukishajiuliza maswali hayo, ndipo uchukue hatua ya kuwa na mwanaume huyo mliyependana.
Kufuatia Wolper kuhusishwa na skendo hiyo, IJUMAA WIKIENDA limechimba ukweli wa ishu hiyo na hapa linakupa ripoti kamili;
WOLPER (33), KIBA (34)
Ukimuacha yule ‘Mkongo wa Wolper’ na staa wa Bongo Fleva, Ali Saleh Kiba ‘King Kiba’ aliyezaliwa mwaka 1986 na sasa ana umri wa miaka 34, wanaume wengine wote ambao Wolper alidaiwa kutoka nao kimapenzi, amewazidi umri.
WOLPER (33) NA JUX (31)
Skendo ya Wolper kutoka kimapenzi na staa wa RnB Bongo, Juma Musa ‘Jux’ siyo ngeni. Wolper mwenye umri wa miaka 33 alidaiwa kutoka kimapenzi na Jux mwenye umri wa miaka 31, hivyo ni mdogo wake aliyempita kwa umri wa miaka miwili.
WOLPER (33), MONDI (31)
Ipo kwenye rekodi za IJUMAA WIKIENDA kwamba, Wolper aliwahi kutajwa kutoka kimapenzi na kinara wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ au ‘Mondi’. Wolper mwenye umri wa miaka 33 alidaiwa kutoka kimalovee na Mondi mwenye umri wa miaka 31, hivyo ni mdogo wake aliyempita kwa umri wa miaka miwili, japokuwa penzi lao halikudumu kwa muda mrefu.
WOLPER (33), HARMO (29)
Staa mwingine wa Bongo Fleva, Rajab Abdul ‘Harmonize’ au ‘Harmo’ alidaiwa kutembea anga za bosi wake, Mondi baada ya kutoka kimapenzi na Wolper.
Wakati akitoka na Wolper mwenye umri wa miaka 33, Harmo mwenye umri wa miaka 29 alikuwa mdogo kwa tofauti ya umri wa miaka minne.
WOLPER (33), BROWN (27)
Wakati wa uhusiano wao, Wolper na Brown ambaye ni mwanamitindo maarufu Bongo, walikuwa gumzo kutokana na kwamba mwanadada huyu alionekana ni mkubwa kuliko dogo huyu.
Wolper mwenye umri wa miaka 33, amempita Brown kwa tofauti ya miaka sita.
WOLPER (33), YOUNG KILLER (26)
Habari kuwa mitandaoni kwa sasa ni tetesi za Wolper huyuhuyu, kudaiwa kutoka kimapenzi na staa wa Hip Hop Bongo, Erick Msodoki ‘Young Killer’. Wawili hawa wanapishana kwa miaka saba, kwani wakati Wolper akiwa na umri wa miaka 33, Young Killer ana umri wa miaka 26.
Je, baada ya hapo safari ya Wolper inaendelea? Muda utasema, tusubiri!
MAKALA: GLADNESS MALLYA