The House of Favourite Newspapers

Yanga Kumjaribu Kipa Wa Serengeti Boys Leo

0
Kipa chipukizi wa Yanga, Ramadhan Kabwili.

KUNA uwezekano mkubwa kwa kipa chipukizi wa Yanga, Ramadhan Kabwili, leo Jumamosi kwa mara ya kwanza akakaa langoni kuichezea timu yake hiyo dhidi ya Ruvu Shooting katika mchezo wa kirafiki kwenye Uwanja wa Azam Complex, uliopo Chamazi jijini Dar es Salaam.

Uwezekano wa Kabwili aliyejiunga na Yanga hivi karibuni akiwa kipa namba moja wa timu ya taifa ya vijana ya Tanzania chini ya miaka 17, Serengeti Boys, kucheza mechi hiyo umekuja kutokana na wenzake kuwa majeruhi.

Makipa Rostand Youthe na Beno Kakolanya wanaopokezana langoni, wote hawakufanya mazoezi ya Yanga juzi na jana Ijumaa kutokana na kuwa majeruhi, hivyo Kabwili ana nafasi kubwa ya kucheza leo.

Daktari wa Yanga, Edward Bavu, ameliambia Championi Jumamosi kuwa: “Makipa wetu wawili Rostand na Kakolanya bado ni wagonjwa lakini wanaendelea vizuri, hivyo katika mechi ya kesho (leo) tunaweza kumtumia Kabwili.

“Matarajio yetu ni kwamba Rostand atakuwa fiti hivi karibuni na ataungana na wenzake haraka iwezekanavyo baada ya kuumia mgongo, wakati Kakolanya yeye akiendelea na matibabu ya goti.”

Leave A Reply