The House of Favourite Newspapers

Yanga Mpeni Muda Lwandamina, Ligi Bado

0
Kocha George Lwandami­na

NIANZE kwa kumshukuru Mungu kwa afya njema aliy­onipatia na ni matumaini yangu upo poa, msomaji wa safu hii.

Joto la Ligi Kuu Bara limeende­lea kupamba moto kufuatia mich­ezo mitatu kuchezwa hadi sasa ambapo kumeonyesha kuwa na ush­indani mkubwa katika kila mechi.

 

Kila timu inahitaji kupata matokeo mazuri hasa katika mechi hizi za awa­li ili kujiweka katika nafasi nzuri zaidi ya msimamo wa ligi. Hali hiyo inasa­babisha upinzani kuongezeka zaidi hivyo kufanya kila mechi iwe ngumu.

 

Hali hii, imeonyesha matokeo to­fauti kwa baadhi ya timu ambazo zimekuwa na uhakika wa kuibuka na ushindi katika mechi fulani fulani hali ambayo inaleta changamoto kubwa kutokana na mabadiliko hayo.

 

Msimu huu ligi inaonekana itakuwa ngumu kutokana na udhamini am­bao umeongezeka kwa kasi katika baadhi ya timu shiriki za ligi kuu hali inayowafanya wachezaji kucheza kwa kujituma kutokana na uhakika wa kupata mahitaji yao, hali am­bayo italeta upinzani wa hali ya juu.

 

Kutokana na hali hiyo, hali im­eonekana tofauti kwa upande wa Yanga ambayo msimu uliopita ilianza vyema mechi za awali ambapo kipindi kama hiki ilikuwa na pointi saba to­fauti na sasa ambapo ina pointi tano.

Hali hiyo imesababishwa kuwe na vuguvugu la kutaka kum­timua kocha George Lwandami­na kutokana na matokeo hayo hali ambayo inaleta sintofahamu.

 

Kumekuwa na tabia kwa baadhi ya timu hususan timu kubwa kuanza ku­timua makocha katika mechi chache pale wanapoona matokeo yanakuwa mabaya hata kama kocha aliwapa­tia mafanikio katika msimu uliopita.

 

Klabu na mashabiki wanatakiwa kuwa wavumilivu hasa pale timu zao zinapoteleza kwenye mechi chache kwa kumpa muda kocha aweze ku­jipanga kwa kutambua tatizo la kikosi chake na kulifanyia kazi.

 

Ni kweli kocha anaajiriwa huku akiwa yupo tayari kufukuzwa waka­ti wowote, lakini katika hili Lwan­damina anapaswa kupewa muda na si kufanya maamuzi ya haraka ambayo kwa asilimia kubwa yat­aigharimu timu katika mambo mbalimbali likiwemo suala la fedha.

 

Kumtolea tathimini kocha ndani ya mechi tatu tu na kufikiria suala la kumtimua si jambo jema kwani litaendelea kuleta madhara zaidi badala ya kujenga kwa kuwa ana­kuwa ameathiriwa kisaikolojia.

Naamini yeye ni kocha mzuri, na anatambua kile ambacho kinatokea katika timu yake ili kuweza kukifanyia kazi, sidhani hata kama na yeye anafu­rahia matokeo hayo, jambo la msingi ni vyema akapewa muda wa mechi kadhaa na ikionekana kuwa hali bado ndipo mchakato uweze ku­fanyika wa hayo mabadiliko, lakini bado nina imani naye ya kuweza ku­fanya vyema kwa kuwa ni kocha bora.

 

Kubadilisha kocha katika kipindi hiki ni sawa na kujiingiza shimoni kwa kuwa kocha mpya atakayeku­ja atakuwa hajui mazingira ya ligi yetu na pia kila kocha huwa na fal­safa yake, hivyo itabidi asome maz­ingira kisha ndiyo aje kukaa sawa.

Mashabiki wanatakiwa wafahamu kuwa, katika mpira kuna matokeo matatu kushinda, kufungwa na ku­toa sare, hivyo kinachotokea katika timu ya Yanga ni matokeo ya kawa­ida na ninaamini kuwa kocha ame­ona upungufu na ataufanyia kazi.

 

Kitu kinachowaumiza mashabiki ni kutokana na mazingira waliyojiwekea kichwani kwamba timu yao ni lazima ishinde kila mechi jambo ambalo si sahihi na wanatakiwa kutambua kuwa hata wapinzani wanaokutana nao wanajiandaa na wanahitaji ushindi, hivyo kujihakikishia ushindi wa moja kwa moja ni sawa na kujipa presha.

 

Nakumbuka katika misimu kad­haa iliyopita, Simba walikuwa wak­ibadilisha makocha mara kwa mara pale walipoona matokeo yana­kuwa mabaya lakini mwisho wa siku timu iliendelea kufanya vibaya zaidi badala ya kufanya vizuri am­bapo kulisababaisha kushindwa ku­upata ubingwa kwa misimu kadhaa.

NA KHADIJA MNGWAI | ACHA NISEME | CHAMPIONI JUMATANO

Leave A Reply