WIKI jana nilizungumzia jinsi ambavyo soka la Tanzania linavyoathiriwa na mfumo wa uendeshaji na hii ni katika ngazi zote, taifa hadi mtaa.
Yawezekana huko nyuma au hata sasa kuna watu walikuwa na mawazo mazuri ya kubadilisha mifumo lakini hawakuwa na nguvu kubwa au hawakuwa na hoja thabiti na yawezekana walipingwa tu kwa kuwa mifumo iliyopo inaneemesha wachache.
Kitu kingine ambacho naweza kusema kisaikolojia wengi hatukuwa tayari kwa mabadiliko, lakini sasa iwe isiwe lazima tukubali madiliko.
Mara kadhaa nimewahi kusema umuhimu wa watu kama Yusuf Manji kwenye michezo hasa soka, tasnia ya fani hiyo haiwezi kuendelea bila kuwa na watu wenye nguvu kiuchumi kama huyu.
Tazama nchi zote zilizoendelea kisoka, kuna watu wenye uwezo wa kifedha wamewekeza huko na wanajua kuna faida wanapata.
Dunia ya sasa hakuna mwekezaji ambaye yupo tayari kumwaga mamilioni kwa kisingizio a n a i p e n d a sana timu. H A K U N A !
Hata Manji wakati ana m w a g a mami l i o n i kipindi kile akiwa nje ya uongozi, najua alikuwa na hesabu zake na ndicho kilichotokea baadaye akaingia kwenye uongozi.
Kwa muda aliodumu Yanga kweli alifanya mambo mazuri na yenye faida kwa klabu, lakini kwa hesabu za kawaida hakukuwa na kitu kinachoitwa ‘financial fairplay’.
Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) kwa nguvu kubwa limekuwa likisisitiza matumizi ya fedha ya soka ndiyo yatumike kuendesha timu na siyo fedha za nje ya Soka zitumike kwa jambo hilo.
Manji alikuwa akiisaidia Yanga kwa asilimia kubwa kwa fedha zake binafsi, ndiyo maana kabla hajaondoka madarakani alitangaza kuidai klabu hiyo mabilioni ya fedha.
Tuwe wa kweli Manji ni mfanyabiashara, hawezi kuendelea kumwaga mamilioni bure kutoka kwenye akaunti binafsi kuingiza klabuni huku akijua hakuna mfumo sahihi wa kurejesha na ikiwezekana kupata faida.
Juzi katika kikao baadhi ya wanachama walionekana wakitaka Manji arejee klabuni, wanapiga kelele hizo kwa kuwa wanajua akirejea neema itakuwepo.
Binafsi niwaambie Wanayanga wanatakiwa kuchukua maamuzi magumu wakati huu na kukubali mabadiliko ya kimfumo kuhusu uendeshaji wa klabu.
Hakuna bilionea au milionea atakayejitokeza katika Yanga ya sasa amwage mamilioni akiwa hana uhakika fedha zake zitarudi kwa njia gani.
Zile hadithi za kina fulani tuliokuwa tukisikia wanamwaga fedha klabuni kwa gia ya ufadhili huku upande wa pili wakitumia klabu ‘kufanya yao’ hazipo kwa kuwa dunia hii ya ‘dot. com’ ni rahisi kuaibika pindi unapofanya ujanjaujanja.
Mohammed Dewji anatumia nguvu kubwa kuwekeza ndani ya Simba kwa kuwa ameona wamekubali mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji na anaona kila kitu kikienda sawa kutakuwa na neema kwa kuwa anatambua nguvu ya soka la sasa ilivyo.
Hivyo, ndugu zangu wa Yanga, mkitengeneza mfumo mzuri wa uendeshaji kwanza wababaishaji wanaopigiwa kelele klabuni wataondoka wenyewe tu bila kufukuzwa, matajiri kama kina Manji watajitokeza wenyewe tena kwa wingi na siyo kuwalilia kila siku kwenye vyombo vya habari.
Napongeza Kamati maalum iliyoteuliwa kuongoza klabu hiyo hasa kipindi hiki cha mpito, lakini lazima kuwe na mikakati sahihi ya muda mrefu, japokuwa nimebaki na maswali kuhusu uwajibikaji wa kamati ya utendaji iliyopo madarakani hadi kufikia kuteuliwa kwa kamati hiyo maalum.
Vuvuzela na JOHN JOSEPH Mawasiliano +255 713 393 542
Comments are closed.