The House of Favourite Newspapers

Yanga wasaka mabeki wawili Rwanda, Mauritius

KLABU ya Yanga ipo kwenye mazungumzo na meneja wa mshambuliaji wa Simba, Mnyarwanda, Meddie Kagere ambaye ni Patrick Gakumba kwa ajili ya kuwaletea mabeki wa pembeni wawili kutoka nchi za Rwanda na Mauritius.

Jeuri hiyo ya Yanga wanaipata kutokana na fedha wanazozikusanya kupitia michango yao ya mashabiki wanayoendelea kuikusanya kutoka kwa kamati maalum ya uhamasishaji wa ukusanyaji fedha iliyo chini ya Naibu Waziri, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Anthony Mavunde.

 

Kamati hiyo imeweka maazimio ya kukusanya shilingi bilioni 1.5 ambayo hivi sasa tayari imefanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi milioni 500 kutoka kwa baadhi ya wabunge, viongozi, wafanyabiashara na Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Gakumba alisema kuwa mabeki hao mmoja ni wa kulia kutoka Polisi Rwanda na mwingine wa kushoto kutoka Mauritius ambao wote majina yao ni siri na itajulikana baada ya kukamilisha taratibu zote.

Gakumba alisema, tayari amefanya mazungumzo na mabosi na Yanga na kuahidi kuwasajili mabeki hao kwa mujibu wa mapendekezo ya Kocha Mkuu wa timu hiyo, Mkongomani, Mwinyi Zahera katika kukiimarisha kikosi chake kwenye msimu ujao.

 

Aliongeza kuwa, wakati wowote atatua nchini kwa ajili ya kuzungumza na mabosi hao walioonyesha nia ya kutaka kuwasajili mabeki hao walio chini yake.

“Yanga wanaonekana hivi karibuni watakuwa vizuri kifedha kutokana na ahadi kubwa waliyonipa mabosi wa timu hiyo na kuniomba niwaletee mabeki wawili wa pembeni wa kushoto na kulia.

 

“Mabeki hao wapo na wazuri kiukweli hawatajutia kama wakitua kuichezea Yanga, mmoja ni kutoka Rwanda na mwingine kutoka Mauritius, kikubwa wao waweke fedha nzuri mezani itakayowashawishi wachezaji hao kusaini.

“Mabosi hao nimezuia kuzungumza nao kwa njia ya simu na kuwataka kuwa wakiwa tayari waniambie nije huko nchini kuzungumza na kama tukifikia muafaka mzuri, basi watakuja wachezaji hao,” alisema.

Comments are closed.