The House of Favourite Newspapers

Yanga Yahaha Kupata ITC Za Makambo, Klaus

Mshambuliaji Heritier Makambo (Kulia).

KLABU ya Yanga imeendelea kusotea vibali vya wachezaji wake wa kimataifa, mshambuliaji Heritier Makambo na kipa Klaus Kindoki waliowa-sajili hivi karibuni kufuatia vibali vyao kutoka-milika hadi sasa kutokana na Chama cha Soka cha Congo (Fecofa) kuchelewa kuvitoa.

 

Makambo aliyetokea FC Lupopo alishindwa kucheza mechi ya kimataifa dhidi ya Gor Mahia ya Kenya katika mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika hatua ya makundi kutokana na kutokuwa na ITC ambapo Yanga ilijikuta ikipokea kipigo cha mabao 3-2.

 

Wachezaji hao ni miongoni mwa wachezaji wapya sita waliosajiliwa ndani ya Yanga msimu huu wakiwemo Mrisho Ngassa na Deus Kaseke waliorejea kundini huku wengine ni Jafary Mohamed na Mohamed Issa.

 

Akizungumzia hilo, Ofisa Habari wa Yanga, Dismas Ten ameeleza kuwa wanasubiria majibu ya maombi yao ya ITC kutoka Fecofa waliyoomba ili kuweza kufanikisha zoezi hilo.

 

“Bado ITC za wachezaji wetu wa kimataifa Makambo na Klaus hatujazipata na ndiyo maana walishindwa kucheza katika mchezo uliopita na kwa sasa tunaendelea na mchakato ili kuweza kufanikisha zoezi hilo.

 

“Tumeziomba ITC hizo kupitia Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ambao wao wanawasiliana na Fecofa ili kuweza kukamilisha zoezi hilo ambapo kwa sasa tunawasubiria watume,” alisema Ten.

STORI NA KHADIJA MNGWAI, CHAMPIONI

Comments are closed.